CHANGAMOTO NDANI YA MFUMO WA SISO NA KATANI LTD


Mkuu wa Mkoa wa Tanga Martin Shigela akizungumza na wakulima Shamba la Mkonge Hale, Korogwe (hawapo pichani) alipofanya mkutano hivi karibuni kusikiliza changamoto za wakulima hivi karibuni.
Wakulima wa mkonge Shamba la Hale, Korogwe, wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Tanga Martin Shigela (hayupo pichani) alipofanya mkutano hivi karibuni kusikiliza changamoto za wakulima hivi karibuni.

Na Yusuph Mussa - Tanga

Pamoja na Mfumo wa Wakulima Wadogo wa Mkonge (SISO) kupata mafanikio, bado kuna changamoto kadhaa ambazo sasa zinafanyiwa kazi. Lakini bado, baadhi ya changamoto hixo zilianza kufanyiwa kazi kama anavyoeleza Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Katani Ltd Juma Shamte.

Shamte alitaja baadhi ya changamoto kwenye sekta ya mkonge na mfumo wa SISO ikiwa ni pamoja na uvamizi wa maeneo ya mashamba na hujuma za uchomaji moto wa misitu na
mkonge, hivyo kusababisha mapato kupotea, mfano mioto mikubwa ilitokea kwenye mashamba ya Hale, Magunga na Ngombezi kati ya Mwaka 2014 na 2015, na kukosesha kampuni na wakulima mapato ya sh. bilioni 8.97. 

"Ugumu wa upatikanaji wa mikopo yenye masharti yanayofaa kwa sekta ya mkonge, riba ambayo ni chini ya asilimia 10; kipindi cha uafueni cha zaidi ya miaka mitatu na kipindi cha marejesho cha zaidi ya miaka saba pamoja na kutohitajika dhamana ya asilimia 125. Dhamana iwe shamba la Mkonge na mapato yake. Tija ndogo ya mashamba ya wakulima (tani 0.7 kwa hekta badala ya tani 1.5 kwa hekta na upandaji chini ya mpango, kwani asilimia 71 ya wakulima wamepanda chini ya hekta sita hasa Shamba la Magunga na Mwelya ambayo hufanya viwanda visitumike kikamilifu. Kwa sasa vinatumika  wastani wa asilimia 37, hivyo kuongeza gharama.

"Kukosekana kwa ruzuku na huduma kutoka Serikalini ya gharama za ugani na pembejeo kwa kama inavyotolewa kwenye mazao mengine. Wakulima kwa sasa wanalipia gharama ya maafisa ugani. Uchanga wa vyama vya wakulima wa kukosa ujuzi na uzoefu wa masuala ya kifedha, utawala bora, uwekaji kumbukumbu na ukokotoaji wa gharama za uwekezaji na uendeshaji za mkulima unaleta udhaifu wa kusimamia kikamilifu shughuli za mkulima na kutoa taarifa sahihi kwa wakati. Huduma ya Ushirika ya ukaguzi na usimamizi pia ni ndogo katika kutoa elimu kwa wakulima ya 
ujasiriamali, uchumi na masoko" alisema Shamte.

Changamoto nyingine ni kuingiliwa kwenye sekta ya mkonge na wizi wa majani ya mkonge ya wakulima unaofanywa na walanguzi wasiokuwa na mashamba na viwanda hadi kusababisha kushuka kwa viwango vya ubora wa singa kwa kuchakachua 
mkonge na kuruhusiwa kufanya ulanguzi na watendaji wa Bodi ya Mkonge Tanzania kinyume na kanuni za mkonge za kimataifa, ni moja ya sababu kubwa zinazoleta tofauti kati ya Wakulima na Katani Ltd.

Changamoto nyingine ni dhana potofu kushereheshwa kuliko hali halisi kuhusu malengo, manufaa na  maendeleo ya SISO na Katani Ltd, kutokana na uhaba wa elimu kwa wadau ya uendeshaji wa mfumo wa SISO. Pia Katani Ltd kutokulipwa kwa wakati huduma na mikopo iliyoitoa kwa wakulima yenye thamani ya sh. bilioni 3.8 na kwa Serikali yenye thamani ya sh. bilioni 1.2 iliyochelewa zaidi miaka 15.

UTEKELEZAJI WA MGAWANYO WA MAPATO KWENYE MFUMO WA SISO

Lengo la maboresho kupitia utaratibu wa mgawanyo wa mapato ni kuimarisha  misingi ya mfumo wa SISO ya kuuza pamoja, kuweka kumbukumbu na kutoa  taarifa sahihi kwa wakati pamoja na kugawanya majukumu na mapato ya mkulima na kiwanda kwa asilimia ya utekelezaji katika uwekezaji na uzalishaji toka kwenye ‘shamba’. Bodi ya Mkonge Tanzania (TSB), ilipewa jukumu na wakulima na Katani Ltd kumpata mshauri kufanya upembuzi wa utaratibu na kanuni za kukokotoa huu mgawanyo kwa faida ya panda zote.

Kwa kuwa mshauri ameshatoa ya kupata mgawanyo wa mapato,
anatakiwa kuleta kanuni za ukokotoaji wa vipindi tofauti, mapendekezo ya  maboresho ya mikataba iliyopo na ushauri wa mfumo wa kuunganisha wakulima kwenye chombo cha kusimamia maslahi yao na kutumika kununua hisa kwenye  viwanda vya Katani Ltd.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527