KAGERA KUZINDUA KAMPENI YA FURAHA YANGU..RC GAGUTI AWAHAMASISHA WANAUME KUPIMA VVU


Mkuu wa mkoa wa Kagera Brigedia Jenerali Marco Gaguti akiongea na waandishi wa habari wa vyombo mbalimbali ofisini kwake leo juu ya uzinduzi wa kampeni ya upimaji wa VVU na kutumia ARVs mapema ijulikanayo kama Furaha yangu,Pima,Jitambue - Picha na Angela Sebastian - Malunde1 blog
Ofisi ya mkuu wa mkoa wa Kagera Brigedia Jenerali Marco Gaguti kwa kushirikiana na mganga mkuu wa mkoa pamoja na wadau wa huduma za Ukimwi (TACAIDS) mkoani Kagera wanatarajia kuzindua kampeni ijulikanayo kama Furaha yangu,Pima jitambue.

Kampeni hiyo imelenga kuhamasisha wananchi kujitokeza kupima VVU na kuanza kutumia dawa za kufubaza Virusi (ARVs) mapema endapo watabainika kuwa wameathirika.

Mkuu wa mkoa huyo Gaguti ameeleza hayo leo kuwa kampeni hiyo inatarajiwa kuanza Septemba 21 mwaka huu katika viwanja vya mashujaa maarufu Mayunga vilivyopo mjini Bukoba lengo likiwa ni kupeleka ujumbe kwa jamii ya Kagera hususani wanaume kujitokeza kupima VVU.

Alisema baada ya kampeni hiyo kuzinduliwa watakwenda mpaka ngazi ya wilaya hivyo akawashauri wananchi kulipokea zoezi hilo kwa dhamira njema,kujitokeza kwa wingi ili kupima afya zao hari itakayochangia kupunguza maambukizi ambapo kwa sasa kimkoa ni asilimia 6.5 huku kitaifa ikiwa asilimia 5 tu.

Alisema mkoa huu unaungana na Taifa katika Kampeni upimaji wa VVU kama ambavyo ilizinduliwa na Waziri mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa Juni19,mwaka huu mkoani Dodoma na upimaji huu ni bure.

Na Angela Sebastian - Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527