POLEPOLE AMVAA MAKONDA KUWAFANYIA SHEREHE POLISI


 Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM Humphrey Polepole amesema mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda hakupaswa kufanya sherehe na Polisi kwa sababu kuna mahali hali haikuwa shwari na wao walikaa kimya.


Polepole ameyasema hayo leo Septemba 18,2018 alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisi ndogo ya CCM Lumumba jijini Dar es salaam akielezea sababu za ushindi wa majimbo mawili ya Monduli na Ukonga.

Amesema Chadema wanasema Jeshi la Polisi linawasaidia CCM ilihali aliyekuwa mgombea ubunge wa chama chao kwenye Jimbo la Ukonga Asia Msangi alimkwida msimamizi wa uchaguzi mbele ya Polisi na walikuwa wametulia.

"Makonda hakupaswa kufanya sherehe nao kwa sababu kuna mahali sheria ya tume ilikuwa inakiukwa na wao wapo wametulia" amesema Polepole.

Amesema pamoja na yote CCM inathamini uwepo wa vyama vya upinzani na wanataka wakosolewe na kupewa mawazo mbadala.

"Kwa bahati mbaya hawa wenzetu kazi yao ni kukosoa tu" amesema.

Pia, Katibu huyo aliutaka upinzani utambulike kwa itikadi za vyama vyao badala ya kuonekana mtu zaidi ya chama.

"Kama chama kinachojinasibu kuwa ni mpinzanii mkuu na ninachelea kukiita mpinzani na ninashukuru wameshindwa vibaya, ukimtoa yule kiongozi wao na wapambe wake wa karibu Kinabaki nini, ACT Wazalendo ukimtoa mjomba kinabaki nini.”

"Wajenge kwanza itikadi ya vyama vyao itambulike, CCM ni taasisi inayotambulika kiitikadi" amejinasibu Polepole.

Na Kalunde Jamali, Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527