RC HAPI AAHIDI KUBORESHA SEKTA YA UTALII

HAPI%2B1
Mkuu wa Mkoa wa Iringa Bw. Ally Hapi (katikati) akizungumza na baadhi ya wafanyakazi wa kampuni ya Capital Plus Internantional kuhusiana na maandalizi ya Maonesho ya Utalii Karibu Kusini 2018 alipotembelea ofisi za kampuni hiyo jijini Dar es Salaam leo. Kampuni ya Capital Plus International inashirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kuandaa maonesho hayo yanayotarajiwa kufanyika Septemba 26 hadi 30 mwaka huu kwenye Viwanja vya Kihesa Kilolo mkoani Iringa yakihusisha mikoa yote ya Nyanda za Juu Kusini. HAPI%2B2.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa Bw Iringa Bw. Ally Hapi (katikati) akisisitiza jambo wakati wa kikao hicho. Kulia ni Mratibu wa Maonesho hayo kutoka kampuni ya Capital Plus Internantional Bw Clement Mshana.HAPI%2B7.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa Bw. Ally Hapi (kulia)akipokea zawadi ya kikombe maalumu chenye nembo ya Capital Plus Internantional kutoka kwa mfanyakazi wa kampuni hiyo Bi Farida Adam ikiwa ni ishara ya kumkaribisha kwenye ofisi hizo. Capital Plus Internantional inashirikiana na Ofisi ya Mkoa wa Iringa kuandaa maonesho ya Utalii Karibu Kusini 2018. 

HAPI%2B4.
Mratibu wa Maonesho ya Utalii Karibu Kusini 2018 kutoka kampuni ya Capital Plus Internantional Bw Clement Mshana akifafanua jambo kwa Mkuu wa Mkoa wa Iringa Bw. Ally Hapi kuhusu maandalizi ya Maonesho hayo wakati wa kikao hicho.HAPI%2B5.
Mratibu Msaidizi wa Maonesho ya Utalii Karibu Kusini 2018 kutoka kampuni ya Capital Plus Internantional Bw Malela Kassim (katikati) akifafanua jambo kuhusu maandalizi ya Maonesho hayo kwa Mkuu wa Mkoa wa Iringa Bw. Ally Hapi (hayupo pichani)wakati wa kikao hicho.HAPI%2B6.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa Bw. Ally Hapi (kulia)akipokea zawadi ya kikombe maalumu chenye nembo ya Utalii Karibu Kusini kutoka kwa mfanyakazi wa Kampuni ya Capital Plus Internantional (CPI) Irene Lymo ikiwa ni ishara ya kumkaribisha rasmi Mkuu huyo kwenye mkakati wa kutangaza Utalii Nyanda za Juu Kusini sambamba na maandalizi ya Maonesho ya Utalii Karibu Kusini 2018. HAPI%2B3.%2B%25282%2529
Nataka mambo yawe hivi! Ndivyo anavyo maanisha Mkuu wa Mkoa wa Iringa Bw. Ally Hapi wakati akizungumza kwenye kikao hicho.




MKUU wa mkoa wa Iringa Bw. Ally Hapi ameahidi kushirikiana kikamilifu na wakuu wenzake wa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini kutangaza fursa na vivutio vya kiutalii vinavyopatikana katika ukanda huo, ikiwa ni mwendelezo wa harakati za kuunga mkono adhma ya Rais John Pombe Magufuli ya kufungua na kutangaza vivutio vya utalii vinavyopatikana katika ukanda wa Nyanda za Juu Kusini.

Katika kuthibitisha hilo kwa vitendo, Bw Hapi ameahidi kuunga mkono jitihada zilizoanzishwa na mtangulizi wake aliyekuwa Mkuu wa Mkoa huo Bi. Amina Masenza za kuyaboresha zaidi Maonesho ya Utalii Karibu Kusini 2018 yanayoenda sambamba na Maadhimisho ya Siku ya Utalii Duniani ambayo Kitaifa yatafanyika mkoani Iringa Septemba 26 hadi 30 mwaka huu.

Bw Hapi ametaja mkakati wake huo, mapema wiki hii jijini Dar es Salaam alipotembelea Ofisi za Kampuni ya Capital Plus International (CPI) inayoshirikiana na ofisi ya Mkuu wa Iringa pamoja na Wizara ya Maliasili na Utalii kuratibu maonesho hayo yanayofanyika mjini Iringa kwa mwaka wa tatu mfululizo.

“Tungependa watu kutoka maeneo mengine ya Tanzania na hata nje ya nchi waje katika maonesho hayo ili waone na kutembelea vivutio vya utalii, kihistoria na kufahamu fursa za uwekezaji tulizo nazo”, alisisitiza kiongozi huyo wa Iringa.

‘’Mikoa ya nyanda za juu Kusini inasifika kuwa na hifadhi zenye sifa za kipekee ikiwemo Hifadhi ya Taifa ya Ruaha yenye makundi makubwa ya tembo na wanyama wengine. Aidha, hifadhi ya Kitulo yenye aina mbali mbali za maua ambayo hayapatikani mahali pengine Duniani na Udzungwa yenye wanyama na viumbe adimu duniani kama vyura wa Kihansi,’’ alitaja

Alisema mkoa wa Iringa ambao unaratibu maonesho hayo kwa kushirikiana na mikoa jirani ya Mbeya, Njombe, Songwe, Ruvuma, Rukwa na Katavi, umejipanga kushirikiana na sekta ya utalii, sekta binafsi pamoja jamii ya kimataifa ili kuyaboresha.

“Kwa mfano mkoa wetu wa Iringa mbali na vivutio vya hifadhi tuna vivutio vya kihistoria. Inafahamika kuwa mkoa huu kupitia Chifu Mkwawa ulikuwa mstari wa mbele kwenye harakati za kupinga ukoloni hasa wa Kijerumani.’’

“Naamini tukishirikiana vizuri na wenzetu wa Ujerumani tunaweza kupokea watalii wengi zaidi kutoka huko watakaokuja kujifunza mengi ya kihistoria ikiwemo kumjua huyu Mkwawa alikuwa ni mtu wa aina gani,aliyeweza kutumia silaha za jadi akawashinda wajerumani waliokuwa na bunduki na risasi za moto’’, alitaja.

Alitoa wito kwa wadau wa Utalii na maendeleo nchini kumuunga mkono kwa kushiriki kikamilifu kwenye maonesho hayo yatakayoambatana na matukio kadhaa ya kimichezo, kitaaluma na kiutamaduni ili kuongeza tija zaidi katika kufikia malengo ya kuongeza mazao ya utalii katika kanda hiyo.

Akizungumzia maandalizi ya maonesho hayo, Mratibu kutoka kampuni ya Capital Plus International Bw Clement Mshana alisema yanaendelea vizuri na kwa sasa kinachoendelea ni kutafuta ushiriki zaidi wa wadau mbalimbali kutoka mashirika na taasisi za kiserikali, sekta binafsi pamoja na mashirika ya kimataifa ili kufanikisha maonesho hayo kwa ubora uliokusudiwa.

“Mbali na maonesho yenyewe kutakuwa na Kongamano la kujadili masuala ya Utalii na Uchumi litakalofanyika tarehe 27 Septemba, 2018 likihusisha washiriki zaidi ya 300. Vile vile kutakuwa na matukio ya kimichezo yakiwemo mashindano ya mbio za baiskeli, ngoma za asili, huku kilele cha maonesho hayo kikitarajiwa kupambwa na mashindano ya mbio za nyika (marathon) zitakazifanyika Septemba 30 mkoani Iringa,’’ alisema.

Bw Mshana alisema katika kipindi chote cha maonesho hayo umeandaliwa utaratibu wa usafiri kwa washiriki, wageni pamoja na wenyeji wa Mkoa wa Iringa ili waweze kutembelea vivutio vya utalii vilivyopo katika ukanda huo.“Nawaomba sana wananchi wote wajipange kushiriki katika maonesho haya makubwa. Pia niwaombe sana wadau wetu wa maendeleo, ikiwemo sekta binafsi, wajitokeze kwa wingi kuunga mkono maonesho haya.’’ Alisema

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527