TWAWEZA YAIJIBU SERIKALI

SHIRIKA lisilo la kiserikali la Twaweza, limejibu barua ya Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (Costech), iliyowataka kueleza taratibu walizotumia wakati wa kufanya utafiti wa umaarufu wa viongozi wa kisiasa nchini. 

Akizunguma jana na Nipashe kwa njia ya simu, Ofisa Mawasiliano wa Twaweza, Annastazia Rugaba, alisema walijibu barua hiyo tangu Ijumaa iliyopita. 

“Hatuwezi kueleza tulichowajibu kwa kuwa yalikuwa ni mawasiliano kati ya taasisi na taasisi, ila tumeshawajibu kabla ya muda wa siku saba waliotupa,” alifafanua baada ya kutakiwa kueleza majibu yao. 

Nipashe iliwasiliana na Costech kutaka kujua ni lini uamuzi kuhusu shauri hilo utatolewa baada ya Twaweza kujieleza kutokana na kushindwa kufuata taratibu wakati wa kufanya utafiti wa umaarufu wa viongozi wa kisiasa, Kaimu Mkurugenzi wa Costech, Dk. Amos Nungu, alisema maamuzi yoyote yatakayotolewa dhidi Twaweza, hayatakuwa hadharani kwa kuwa yalikuwa mawasiliano ya ndani. 

“Hatutarajii kutoa chochote kitakachojadiliwa nje kwa sababu siyo nia yetu, ilikuwa bahati mbaya kwamba ile barua ilikwenda kwenye mitandao, hivyo hata majibu yatakuwa ndani ya taasisi na taasisi,” alifafanua. 

Aidha, alisema majibu ya barua kutoka Twaweza yalishapokelewa na yanafanyiwa kazi na Costech. Wiki iliyopita, mkurugenzi huyo alisema “Tume inayo kamati maalum inayohusika na kusajili na kutoa vibali kwa tafiti mbalimbali zinazoendeshwa Tanzania. 

Maombi hupelekwa kwa wataalamu waliobobea katika nyanja husika kabla ya kuletwa kwenye kamati ili kujadiliwa. 

Alisema Tume imekuwa ikiwasiliana na wadau pale wanapobaini utafiti kufanyika bila kusajiliwa ama kufuata taratibu na ndiyo maana iliwasiliana na Twaweza. 

Dk. Nungu alisema siyo mara ya kwanza Costech kuwaandikia barua wadau wake na Twaweza siyo wa kwanza kuandikiwa barua ya namna hiyo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527