TUME YA TAIFA YA UCHAGUZI YAWAENGUA WAGOMBEA 15 WA UDIWANI

Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imesema kati ya rufaa 25 zilizokatwa na wagombea wa udiwani, kumi wameshinda na 15 wameenguliwa kushiriki uchaguzi mdogo wa Agosti 12, 2018.

Akizungumza Julai 21, 2018, Mkurugenzi wa NEC, Dk Athumani Kihamia amesema Tume ilipokea rufaa 25 ambazo walizifanyia kazi kwa mujibu wa sheria za uchaguzi.

“Jumla ya wagombea 10 wamerejeshwa katika kinyang’anyiro na 15 rufaa zao hazikufanikiwa, hivyo hawatoendelea kuwa wagombea,” amesema Dk Kihamia.

Amesema katika uchaguzi wa Agosti 12, 2018 kati ya kata 77, wagombea udiwani 30 wamepita bila kupingwa.

Mkurugenzi huyo amesema vyama 11 vinashiriki uchaguzi huo, ACT-Wazalendo ikiwa na wagombea 17 sawa na asilimia 22; ADC watatu sawa na asilimia 3.9 na CCM wako 77 sawa na asilimia 100.

Chadema ina wagombea 54 sawa na asilimia 70 na Chaumma ina wagombea wawili sawa na asilimia 2.6.

Vyama vingine ni, CUF yenye wagombea 17 sawa na asilimia 22; Demokrasia Makini wanne sawa na asilimia 5.2; NCCR-Mageuzi wagombea sita sawa na asilimia nane; NRA watatu sawa na asilimia 3.9; SAU mgombea mmoja sawa na asilimia moja; NRA wagombea watatu sawa na asilimia 3.9; SAU mgombea mmoja sawa na asilimia moja na UPDP wawili sawa na asilimia 2.6

Dk Kihamia amesema katika jimbo la Buyungu, wagombea 10 wa vyama mbalimbali walijitokeza kuchukua fomu za kugombea na wamepitishwa. Kati ya hao, wanaume ni tisa na mwanamke ni mmoja.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527