SIMBA SC YASHUSHA KOCHA MPYA KIMYA KIMYA


Kocha Patrick Aussems (kulia) akiwa na katibu mkuu wa Simba Dr. Anord Kashembe

Mabingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara msimu uliopita, Simba imempokea kimya kimya kocha wao mpya raia wa Ubelgiji, Patrick Aussems ambaye amekuja kuziba nafasi ya Pirre-Lechantre ambaye ameachana na klabu hiyo mwishoni mwa msimu uliopita wa mwaka 2017/18.

Patrick Aussems mwenye umri wa miaka 53 ambaye aliwahi kucheza kama mlinzi enzi za uchezaji wake amekuja nchini mapema Jumapili ya wiki hii na kushuhudia mchezo wa pili wa Simba wa kombe la Kagame ambao waliifunga Rayon Sport 2-1 na jana pia alishuhudia mchezo ambao Simba ilitoka sare na Singida United.

Kocha huyo aliwahi kuzifundisha klabu kadhaa zikiwamo ES Troyes AC na Stade De Reims za Ufaransa pamoja na mabingwa wa kombe la Shirikisho la Afrika mwaka 2012, AC Leopards ya Congo Brazzaville .

Inaelezwa kuwa kocha huyo yupo katika mazungumzo ya mwisho na uongozi wa klabu ya Simba juu ya masuala ya mkataba kabla ya kumwaga wino rasmi kuitumikia klabu hiyo ambayo inashiriki michano ya kimataifa msimu ujao.

Historia yake kwa ufupi .

Jina lake halisi ni Patrick Winand Aussems , alizaliwa mnamo Februari 6, 1965 na alichezea baadhi ya vilabu vikubwa kadhaa barani Ulaya vikiwemo Standard Liege, KRC Gent na RFC Seraing za Ubelgiji, pamoja ES Troyes AC ya Ufaransa.

Mafanikio makubwa ambayo aliyapata ni kuiwezesha klabu ya AC Leopards ya Congo Brazzaville mwaka 2014 kuchukua ubingwa bila ya kupoteza mchezo wowote na kuifikisha katika nusu fainali ya kombe la Shirikisho ambapo ilipoteza mchezo huo mbele ya Sewe Sports ya Ivory Coast katika mwaka huo huo. Pia aliwahi kuifundisha timu ya taifa ya Nepal kati ya mwka 2015-2016.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527