RC KIGOMA ATAHADHARISHA MASHIRIKA NA VIKUNDI VYA WAKIMBIZI

Mkuu  wa Mkoa wa Kigoma Brigedia Jenerali Mstaafu Emanuel Maganga ameyataka mashirika pamoja na vikundi vya Wakimbizi vinavyowashawishi wakimbizi kuacha kujiandisha kurudi kwao kwa hiari kuacha tabia hiyo.

Mkuu huyo alitoa agizo hilo jana wakati akizungumza na wakimbizi katika kambi ya Ndita wilayani Kibondo ambapo alisema Mashirika na vikundi hivyo wanavijua endapo wataendelea na tabia hiyo watachukua hatua za kisheria ikiwa ni pamoja na mashirika yanayochochea wakimbizi na kuunga mkono upinzani nchini Burundi kuwa yataondolewa na hayataruhusiwa kutoa huduma tena.

"Yapo mashirika yanakwamisha zoezi hili tunawajua niwaombe kitu kimoja kama mna maslahi yenu binafsi muyaweke pembeni hatutawavumilia, ukiona shirika lako limeitwa ofisini kwangu jiandae kuondoka na tukifukuza hapo hakuna sehemu tena katika Taznania hii utafanya kazi", alielezea Maganga.

Alisema kwa sasa hali ya amani na usalama kwa nchi ya Burundi ni salama na mali walizoziacha kwao bado zipo hivyo wakimbizi warejee nyumbani kwao kwa kuwa hakuna utaratibu wa mkimbizi wa Burundi kwenda nchi ya tatu kwani utaratibu huo ni kwa Wakongomani pekee.

Alisema kambi ya wakimbizi sio mahali pa kudumu ni mahali pa kuhifadhi raia ambao nchini mwao kuna tishio la kiusalama,  kwa sasa Burundi usalama upo hivyo wananchi wanatakiwa kurejea nchini kwao kwa hiari na kusitokee vitisho wala ushawishi wowote.

"Utaratibu wa kuwapeleka raia wa Burundi nchi ya tatu ni ya haupo na Serikali ya Tanzania haitoi uraia kwa wakimbizi wa Burundi kama njia zote zimefungwa njia iliyopo ni moja tu mrejee kwenu kwa hiari na UNHCR na IOM itahakikisha mnasafiri na mnafika kwenu mnaishi vizuri", alisema Brigedia jenerali Maganga.

Pamoja na hayo baadhi ya Wakimbizi akiwemo Nkruliyabanzi Andrew alisema wao kama wakimbizi wanapenda kurejea nchini mwao lakini bado wanauoga kuwa wanaweza kurudi nchini mwao wakaanza kunyanyaswa kwakuwa walikimbia.

Waliomba serikali ya Tanzania kuzungumza na serikali ya Burundi kuingia kambini kuzungumza na wakimbizi na kuwahahikishia endapo watarudi wataishi salama wao wako tayari kurejea nchini mwao wakihakikishiwa hayo.

Uamuzi wa kuwarejesha wakimbizi walioingia nchini Tanzania 2015 ulifikiwa mwishoni mwa mwaka 2017 baada ya pande tatu za shirika la kuhudumia wakimbizi UNHCR na nchi za Burundi na Tanzania kujiridhisha hali ya usalama Burundi imerejea na kuwaomba wakimbizi warudi kwao ambapo mpaka sasa baadhi ya wakimbizi wamerejea nchini mwao kwa hiari. 

Na Rhoda Ezekiel- Malunde1 blog Kigoma
Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Brigedia Jenerali Mstaafu Emanuel Maganga akizungumza na wakimbizi katika kambi ya Nduta wilayani Kibondo Mkoani Kigoma akiwataka kurejea nchini kwao kwa hiari, pembeni ni watumishi wa idara ya mambo ya ndani na baadhi yamashirika ya kuhudumia wakimbizi - Picha na Na Rhoda Ezekiel- Malunde1 blog



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527