RAIS MAGUFULI : WASIOFURAHIA NDEGE MPYA WATAPATA TABU SANA

. Rais John Magufuli amebainisha sababu za kununua ndege ikiwa ni pamoja na kujenga heshima na kulinda hadhi ya Taifa.


Amesema ilikuwa aibu kwa Tanzania, nchi yenye idadi ya watu zaidi milioni 50 kutokuwa na ndege.


Pia, amesema Watanzania wengi wamefurahia ujio wa ndege hiyo na kwamba, kama wapo ambao hawajafurahia basi watapata tabu sana.

Dk Magufuli amesema hayo leo Julai 8, 2018 akipokea ndege aina ya Boeing 787- 8 Dreamliner iliyowasili saa 11:15 jioni.

Amesema ununuzi wa ndege hiyo ni jitihada za Watanzania wote ambao wanalipa kodi.


Rais ametaja sababu nyingine kuwa ni kuboresha huduma ya usafiri wa ndege nchini kwa sababu Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) lilikuwa na ndege moja pekee yenye uwezo wa kubeba abiria 51.


Amesema Watanzania wengi hawatumii usafiri wa ndege lakini haimaanishi kwamba hawapendi kutumia aina hiyo ya usafiri.


“Hawatumii kwa sababu ndege zilikuwa zinakwenda miji mitatu pekee, lakini sasa wanatua kwenye miji 12," amesema Rais Magufuli.


Amesema pia gharama zilikuwa kubwa, hivyo ujio wa ndege hiyo utapunguza gharama za usafiri na wananchi wa kawaida wataweza kusafiri.


Rais Magufuli amesema sababu nyingine ni kukuza sekta ya utalii nchini.


"Tunataka tuwe tunafanya safari za kimataifa. Ninaamini tukianza na ndege hii na ile nyingine ikija, ni wazi kwamba idadi ya watalii nchini itaongezeka," amesema.


Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi John Kijazi amesema ununuzi wa ndege una manufaa makubwa ambayo ni pamoja na kuimarisha mtandao wa usafiri nchini.


"Ndege hizi zitaimarisha biashara, uwekezaji na utalii nchi. ATCL zitunzeni ndege na muweke mipango mizuri ya biashara na kuilipa serikali fedha za ukodishaji kwa mujibu wa mkataba," amesema Balozi Kijazi.


Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Leonard Chamliho amesema ndege ya Dreamliner itaanza safari katika miji ya Dar es Salaam, Kilimanjaro na Mwanza ili kuwapa uzoefu marubani.


Amesema Septemba, 2018 ndege hiyo itaanza kwenda Bombay (India), Bangkok (Thailand) na Guangzhou (China).


Pia, amesema wameanza mchakato ili ndege hiyo iwe inatua Uingereza.
Chanzo- Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527