MAGUFULI : HAKUNA MBADALA WA CCM...WANAOHANGAIKA WATAPATA TABU SANA

Rais na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt. John Magufuli amefunguka na kudai chama hicho kitaendelea kutawala milele na milele huku akiwapiga vijembe upinzani kuwa watapata tabu sana siku zote kushindana na chama hicho.


Dkt. Magufuli ametoa kauli hiyo leo Julai 16, 2018 wakati alipokuwa anahutubia mamia ya wakazi wa Mkoa wa Pwani, Kibaha waliojitokeza kushuhudia zoezi la kuweka jiwe la msingi la Chuo cha Uongozi cha Mwalimu Julius Nyerere ambacho kitakuwa kina kazi kubwa ya kuwapika wanasiasa nchini Tanzania na Afrika kiujumla.

"CCM ni chama tawala na kitaendelea kutawala milele na milele, wanaohangaika watapata tabu sana siku zote. Chama hiki kipo na kitaendelea kuwepo na kitaendelea kuleta maendeleo kwa ajili ya watanzania. hakuna mbadala wa CCM", amesema Dkt. Magufuli.

Pamoja na hayo, Dkt. Magufuli ameendelea kwa kusema "kwa wananchi na wanachama wa CCM tembeeni kifua mbele. Tumeamua kuleta Tanzania ya kisasa zaidi na yenye maendeleo, viwanda, muelekeo Tanzania inayoshirikiana na vyama vingine katika Afrika. Tanzania inayowapigania wananchi hasa wanyonge ili waweze kushiriki maendeleo yao. Tanzania inayopiga vita rushwa, unyonyaji pamoja na uonevu".

Kwa upande mwingine, Dkt. Magufuli amesema chuo hiko hakitakuwa na ubaguzi wa aina yoyote ile huku akielekeza kuwa chuo hicho kiwe na dira ya waafrika wote na kuleta ukumbozi wa maendeleo ya kiuchumi ndani ya Tanzania.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527