HISTORIA ITAWABEBA ENGLAND KWA CROATIA LEO?

NUSU fainali ya leo kati ya England dhidi ya Croatia inaweza kuwa ya kisasi na kutengeneza historia kwa England ambao wameonekana kuwa wababe kwa wapinzani hao.

Katika historia, timu hizo zimekutana mara saba na leo hii itakuwa ya nane, kati ya hizo England wamekuwa wababe kwa kushinda mara nne, kutoa sare mara moja huku Croatia wakishinda mara mbili.
England hawana historia nzuri ya Kombe la Dunia katika kipindi cha miaka ya hivi karibuni, mara ya mwisho kuingia hatua ya nusu fainali ilikuwa mwaka 1966, ambapo waliweza kutwaa ubingwa moja kwa moja, tangu hapo wamekuja kufanya hivyo mwaka huu nchini Urusi kuingia nusu fainali.
Kizazi cha sasa cha England kina kiu kubwa ya mafanikio ya michuano hiyo ili kuandika historia ambayo baadhi ya mastaa waliopita ndani ya timu hiyo walishindwa, kama vile David Beckham, Steven Gerrard, Frank Lampard, John Terry, Wayne Rooney na wengine wengi.
Katika soka, historia haina nafasi kubwa sana japokuwa timu husika inakuwa inaingia uwanjani huku ikitambua kwamba wapinzani wao ni vibonde.
Soka la sasa linaangalia ubora wa kikosi husika pamoja na mifumo mizuri ya mwalimu ndio ambayo inapewa nafasi kubwa ya kufanya vizuri.
Croatia wanapewa nafasi ya kufanya vizuri katika mchezo wa leo kutokana na kuwa na wachezaji wenye uzoefu na walio bora kwa kipindi cha hivi karibuni kama vile Mario Mandzukic, Mateo Kovacic, Ivan Perisic, Ivan Rakitic, Luka Modric na wengineo.
Kwenye hatua ya makundi, Croatia walicheza soka la kiwango cha hali ya juu katika mchezo wao dhidi ya Argentina na kufanikiwa kushinda mabao 3-0 na hapo ndipo wakapewa nafasi kubwa ya kufika mbali.
Hata hivyo, Croatia walipambana kuhakikisha wenyeji wa michuano hiyo, Urusi wanaondoka katika hatua ya robo fainali kwa mikwaju ya penalti 4-3 baada ya dakika 120 kumalizika kwa sare ya 2-2.
Hivyo, mchezo wa leo utakuwa na ushindani wa hali ya juu kuanzia mbinu za makocha pamoja na uwezo binafsi wa wachezaji.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527