Picha : DC SHINYANGA AIBUKIA STENDI YA MABASI MAADHIMISHO SIKU YA MAZINGIRA DUNIANI

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mheshimiwa Josephine Matiro ametembelea maeneo ya kituo cha mabasi yaendayo wilayani ‘Stendi ya Mjini Shinyanga’ kukagua mazingira ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya siku ya mazingira duniani ambayo hufanyika Juni 5 kila mwaka.

Mkuu huyo wa wilaya akiwa ameambatana na Afisa Mazingira wa Manispaa ya Shinyanga Ezra Manjerenga na wadau mbalimbali wa mazingira ametembelea stendi hiyo leo Jumanne Juni 5,2018.

Baada ya kutembelea eneo hilo,Mheshimiwa Matiro ameeleza kutoridhishwa na hali ya usafi wa mazingira ya stendi hiyo na kuwaagiza viongozi wa halmashauri ya manispaa ya Shinyanga na Kituo hicho cha mabasi kurekebisha mara mapungufu yaliyopo ikiwemo kukosekana kwa vyombo vya kuwekea uchafu ‘dustbin’ na vyoo vichafu.

“Maafisa afya, afisa mazingira,afisa biashara wa manispaa ya Shinyanga na wafanyabiashara mliopo katika stendi hii nawapa wiki moja hakikisheni kuna vifaa vya kuwekea uchafu,zuieni watu wanaokojoa ovyo hapa na wanaotupa makopo ya mikojo na hivi vyoo viboresheni,wekeni utaratibu mzuri na mhakikishe vinakuwa visafi”,alisema Matiro.

“Ni jukumu la kila mmoja kutunza mazingira,yeyote anayechafua mazingira mchukulieni hatua za kisheria,tunataka wananchi wawe salama kiafya,mkiwa na afya bora mtaendelea kufanya shughuli za kiuchumi na bila afya bora hatuwezi kufikia uchumi wa kati na Tanzania ya viwanda”,aliongeza Matiro.

Kwa upande wake,Mwenyekiti wa Umoja wa wafanyabiashara katika stendi hiyo,Rashidi Issa alisema changamoto wanayokutana nayo ni mabasi yanayotoka jijini Dar es salaam ambayo hulala katika stendi hiyo ambapo abiria wamekuwa wakijisaidia katika makopo ya maji kisha kutupa mikojo katika stendi hiyo hivyo kuiomba serikali kuwapatia askari polisi ambao watakuwa katika stendi hiyo muda wote kudhibiti wachafuzi wa mazingira.

Naye Afisa Mazingira wa manispaa ya Shinyanga,Ezra Manjerenga aliwahamasisha wananchi kupanda miti na kutumia nishati mbadala kama vile matumizi ya gesi badala ya kujikita kwenye matumizi ya nishati ya mkaa.

“Kauli mbiu ya taifa ya maadhimisho ya siku ya Mazingira duniani mwaka huu ni ‘Mkaa ni gharama tumia nishati mbadala’,hivyo nawaomba mtumie nishati zingine kama gesi ili kupunguza gharama lakini pia itasaidia katika kutunza mazingira yetu”,alisema Manjerenga.

Awali kabla ya kwenda katika kituo cha mabasi yaendayo mikoani, Afisa Mazingira wa manispaa ya Shinyanga,Ezra Manjerenga aliongoza zoezi la kufanya usafi katika barabara mbalimbali mjini Shinyanga akiwa ameambatana na Mtaalamu wa takataka kutoka Ujerumani Dorothea Kruse,vijana wa skauti na wadau mbalimbali wa mazingira katika manispaa ya Shinyanga.

ANGALIA PICHA ZA MATUKIO HAPA CHINI
Kulia ni Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mheshimiwa Josephine Matiro akizungumza na wafanyabiashara katika kituo cha mabasi yaendayo wilayani 'Stendi ya Shinyanga Mjini' na kuwahamasisha kutunza mazingira wakati wa maadhimisho ya siku ya mazingira duniani leo Juni 5,2018.Wa kwanza kushoto ni Mwenyekiti wa Umoja wa wafanyabiashara katika stendi hiyo,Rashidi Issa- Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog 
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mheshimiwa Josephine Matiro akizungumza na wafanyabiashara na wasafiri katika Stendi ya Shinyanga Mjini.
Wananchi wakimsikiliza mkuu wa wilaya ya Shinyanga mheshimiwa Josephine Matiro.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mheshimiwa Josephine Matiro akizungumza na wafanyabiashara na wasafiri katika Stendi ya Shinyanga Mjini.

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mheshimiwa Josephine Matiro katika Stendi ya Shinyanga Mjini.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mheshimiwa Josephine Matiro akiwa katika Stendi ya mabasi ya Shinyanga Mjini akielekea katika choo kilichopo katika stendi hiyo.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mheshimiwa Josephine Matiro akiwa katika choo cha wasafiri katika stendi ya mabasi Mjini Shinyanga.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mheshimiwa Josephine Matiro akiwa ndani ya choo cha stendi ya mabasi mjini Shinyanga na kubaini kuwa ni vichafu hivyo kuagiza vifanyiwe usafi.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mheshimiwa Josephine Matiro akiangalia kipande cha diaba kinachotumika kutunza taka katika choo kilichopo katika stendi ya mabasi ya Shinyanga Mjini na kuagiza kuwekwa vifaa maalum kwa kuwekea uchafu 'dustbin'.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mheshimiwa Josephine Matiro akiondoka katika choo kilichopo katika stendi hiyo ya mabasi.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mheshimiwa Josephine Matiro akikatisha katika Uchochoro kuelekea katika choo kingine kilichopo nyuma ya  Stendi ya mabasi yaendayo wilayani 'Stendi ya Shinyanga mjini' ambacho nacho hali yake ni mbaya,kichafu,kuna nyufa za kutisha hali inayohatarisha afya za wananchi katika eneo hilo.
Choo kilichopo nyuma ya Stendi ya mabasi ya Mjini Shinyanga ambacho hali yake ni mbaya,kichafu,kuna nyufa za kutisha hali inayohatarisha afya za wananchi katika eneo hilo.Katika hali ya kushangaza baadhi ya vyumba vya choo vimegeuzwa vyumba vya kulala watu.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mheshimiwa Josephine Matiro akishangaa jinsi choo hicho kilichochakaa na kuagiza kikarabatiwe ama huduma isitishwe kwa ajili ya usalama wa wananchi.
Moja ya vyumba vya choo kinachotumiwa 'kulala watu'
Mheshimiwa angalia paleee huwa wanamwaga maji machafu na kukojoa..... Mwananchi akimuonesha mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mheshimiwa Josephine Matiro eneo ambalo limegeuzwa choo.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mheshimiwa Josephine Matiro akimpa maelekezo Afisa biashara manispaa ya Shinyanga Sunday Deogratius (kulia) kukutana na wafanyabiashara wa eneo la stendi kujadili namna ya kumaliza kero zilizopo.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mheshimiwa Josephine Matiro akiendelea kumpa maelekezo Afisa biashara manispaa ya Shinyanga Sunday Deogratius. 
Afisa Mazingira wa Manispaa ya Shinyanga Ezra Manjerenga akiwaelezea wafanyabiashara na wasafiri katika stendi ya mabasi yaendayo wilayani kuhusu maadhimisho ya siku ya mazingira  duniani.
Afisa Mazingira wa Manispaa ya Shinyanga Ezra Manjerenga akizungumza katika stendi ya mabasi yaendayo wilayani
Kushoto ni Mtaalamu wa takataka kutoka Ujerumani Dorothea Kruse akiwashukuru wakazi wa Shinyanga kwa kujitokeza kufanya usafi maeneo mbalimbali mjini Shinyanga leo wakati wa maadhimisho ya siku ya mazingira duniani
Kamishna  wa skauti wilaya ya Shinyanga Peter Mgalula akiwashukuru vijana wa skauti kwa kushiriki katika zoezi la kufanya usafi katika maeneo mbalimbali mjini Shinyanga leo wakati wa maadhimisho ya siku ya mazingira  duniani.
Kijana akitoa burudani ya wimbo katika stendi ya mabasi yaendayo wilayani leo wakati wa maadhimisho ya siku ya mazingira duniani.
Kijana mwingine akitoa burudani ya wimbo
Vijana wa skauti wakiwa na bango linalosomeka 'Shinyanga mpya mti kwanza, Mkaa ni gharama,tumia nishati mbadala'
Wadau wa mazingira wakiongozwa na Afisa Mazingira wa manispaa ya Shinyanga,Ezra Manjerenga wakikusanya uchafu katika eneo la Mazingira Centre mjini Shinyanga.
Wadau wa mazingira wakikusanya uchafu katika eneo la Hospitali ya rufaa ya mkoa wa Shinyanga.
Wadau wa mazingira wakiendelea kutafuta uchafu mjini Shinyanga.Kushoto ni Mtaalamu wa takataka kutoka Ujerumani Dorothea Kruse.


 Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog 

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527