WAZIRI MKUU APIGWA MARUFUKU KUSAFIRI NJE YA NCHI

Waziri Mkuu wa zamani Najib Razak na mkewe Rosmah Mansor wamezuiwa kuondoka nchini, Idara ya Uhamiaji imesema leo Jumamosi.


Taarifa ya Idara ya Uhamiaji ilitolewa muda mfupi baada ya kiongozi huyo wa zamani mwenye kashfa ya ufisadi kuandika katika Facebook kwamba yeye na familia yake wanatarajiwa kwenda ughaibuni kwa mapumziko kuanzia Jumamosi na watarejea wiki ijayo.


Katika akaunti ya Twitter Najib amesema ataheshimu amri ya kuzuiwa iliyotolewa na serikali kumtaka asiondoke nchini.


"Nimetaarifiwa kwamba Idara ya Uhamiaji imenizuia mimi na familia yangu kusafiri nje ya nchi. Naheshimu amri na nitabaki nchini na familia yangu,” ameandika Najib.


Waziri mkuu huyo aliyeondolewa kupitia sanduku la kura sasa anachunguzwa na Serikali juu ya tuhuma za ufisadi wa fedha za uwekezaji ambazo maofisa wanadaiwa kuiba zaidi ya dola za Marekani 4.5bilioni.


Inadaiwa kiasi kingine cha fedha kiliishia kwenye akaunti binafsi ya Najib katika benki.


Najib amekanusha kufanya kosa lolote na anasema fedha hizo zilitolewa na familia ya kifalme ya Saudi Arabia na kwamba alikwisharejesha.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527