Shirika la Ariel Glaser Pediatric Aids Healthcare Initiative (AGPAHI), limewakutanisha wadau wa mapambano dhidi ya Virusi vya Ukimwi na Ukimwi mkoani Mwanza ili kwa pamoja kujadili na kuboresha shughuli mbalimbali zinazofanywa na wadau hao.
Afisa Mradi Huduma Unganishi kwa Jamii kutoka shirika la AGPAHI mkoani Mwanza, Cecilia Yona amesema huo ni mkutano wa robo mwaka na unawashirikisha wadau wanaotoka katika vikundi vya kijamii (CBO) vinavyosaidia mapambano dhidi ya Virusi vya Ukimwi na Ukimwi.
Amesema lengo la mkutano huo ni kusikiliza na kujadili shughuli mbalimbali zinazofanywa na wadau hao na kuweka mikakati ya kuboresha huduma za tiba na matunzo kwa wateja wanaopata huduma katika vituo vya CTC.
Baadhi ya washiriki wa mkutano huo wamebainisha kwamba wamekuwa na jukumu kubwa la kuhakikisha wanawahamasisha wanajamii kuwa tayari kupima virusi vya Ukimwi na pia kuondokana na hali ya unyanyapaa.
Mkutano huo wa siku mbili kuanzia jana April 30, 2018 unafanyika Adden Palace Hotel Pasiansi Jijini Mwanza, ukihusisha washiriki kutoka wilaya za Nyamagana, Ilemela, Ukerewe pamoja na Sengerema ambapo shirika la AGPAHI limekuwa likifanya shughuli zake hapa nchini kwa ufadhili wa serikali ya Marekani kupitia shirika la Centres for Disease Control (CDC).
George Binagi-GB Pazzo @BMG
Afisa Mradi Huduma Unganishi kwa Jamii kutoka shirika la AGPAHI mkoani Mwanza, Cecilia Yona akizungumza kwenye mkutano huo. Mratibu wa Kudhibiti Ukimwi wilaya ya Nyamagana, Erica Steven akizungumza kwenye mkutano huo. Washiriki wa mkutano huo. Bonyeza HAPA kwa habari zaidi.