PINGAMIZI KESI YA UCHOCHEZI YA VIGOGO WA CHADEMA LATUPILIWA MBALI

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, imetupilia mbali pingamizi la awali la upande wa utetezi katika kesi ya uchochezi inayowakabili viongozi wa CHADEMA akiwemo Mwenyekiti wake Freeman Mbowe ya kutaka kesi yao isikilizwe Mahakama Kuu.


Uamuzi huo umetolewa na Hakimu Mkazi Mkuu, Wilbard Mashauri baada ya Wakili wa serikali Mkuu, Faraja Nchimbi kueleza kuwa shauri hilo limeitishwa kwa ajili ya kutolewa uamuzi.


Hakimu Mashauri amesema kuwa amepitia hoja zote za utetezi na upande wa mashtaka, ambapo ameona hoja za upande wa mashtaka hazina mashiko.


“Natupilia mbali hoja za upande wa mashtaka kwamba kesi iende Mahakama Kuu,” amesema ambapo ameahirisha kesi hiyo hadi May 16,2018 kwa ajili ya washtakiwa kusomewa Ph.


Miongoni mwa hoja za utetezi kutaka kesi hiyo ipelekwe Mahakama Kuu ni kwa sababu kuna uvunjifu wa haki ya msingi ya Kikatiba.


Pia shtaka la pili linalowakabili washtakiwa katika hati ya mashtaka linakiuka haki ya msingi ya washtakiwa ya kufanya shughuli za kisiasa za chama wanachotoka cha CHADEMA.


Katika kesi hiyo, washtakiwa wanakabiliwa na jumla ya mashtaka 12 ikiwamo kula njama, kufanya mkusanyiko usio halali kinyume cha sheria na kuendelea kufanya mkusanyiko usio halali ama maandamano yaliyosababisha kifo cha Akwilina Akwiline.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527