MWANAFUNZI WA CHUO AHOFIWA KUTAFUNWA NA MAMBA AKICHOTA MAJI MTONI

Mwanafunzi wa Chuo cha Taaluma ya Wanyamapori Pasiansi kilichopo jijini Mwanza, Wambura Otaigo (19) anahofiwa kufa maji baada ya kuzama ndani ya Mto Grumeti wilayani hapa mkoani Mara wakati wanachota maji ya matumizi kambini.


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara, Juma Shija alisema tukio hilo lilitokea Aprili 23 na hadi sasa mwanafunzi huyo hajaonekana.


Mto Grumeti unamwaga maji Ziwa Victoria, hivyo kuibua hofu ya mwili wa mwanafunzi huyo kutopatikana kutokana na wingi wa maji unaotokana na mvua za masika zinazonyesha sehemu mbalimbali nchini.


Kamanda Shija alisema wakati wa tukio hilo mwanafunzi huyo aliyekuwa kwenye mafunzo kwa vitendo katika Kituo cha Mazoezi cha Fort Ikoma wilayani Serengeti, alikuwa na wenzake ambao walijaribu bila mafanikio kumsihi asiingie majini kutokana na mto kufurika na maji kutiririka kwa kasi.


Mto Grumeti unadaiwa kuwa na idadi kubwa ya mamba, hali inayozidisha hofu ya mwanafunzi huyo kupatikana licha ya juhudi za askari polisi, wanafunzi wenzake pamoja na wananchi za kumtafuta.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527