SERIKALI YA TANZANIA YABARIKI DAWA YA ASILI MAARUFU "UJANA" KUTIBU NGUVU ZA KIUME


SERIKALI imesema haijawekeza kwa kiwango kikubwa katika afya ya mwanamume upande wa afya ya uzazi, lakini zipo tafiti mbalimbali zikiwemo za nje ya nchi, ambazo zimekuwa zikionesha kuwepo kwa hali ya kushuka kwa nguvu za kiume.

Hata hivyo, imesema ipo dawa ijulikanayo kama ‘Ujana’ ambayo imesajiliwa na Baraza la Usajili wa Tiba Asili na Tiba Mbadala, ambayo inalenga katika kuongeza nguvu za kiume.

 Imesema upo utafiti kuhusu afya ya wanaume, unaofanywa na Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMRI), ambao umefikia katika hatua nzuri, ambayo ni katika ufungashaji. 

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Faustine Ndugulile alisema hayo Dar es Salaam jana wakati akizungumzia usajili wa dawa za tiba asili na tiba mbadala.

Ndugulile alisema Tanzania haijafanya utafiti kuhusu eneo hilo la afya ya uzazi kwa wanaume, kama ilivyo kwa hali ya uzazi kwa wanawake na watoto nchini, lakini ili kujua tatizo lipo kwa kiwango gani licha ya kwamba takwimu za kidunia zinazoonesha eneo hilo kuwa tatizo.

 Alitaja sababu zinazochangia kupungua kwa nguvu za kiume kuwa ni kutofanya mazoezi, ulaji wa vyakula visivyo bora kiafya na kula vyakula vyenye mafuta kwa wingi.

 Nyingine ni utumiaji wa vilevi ikiwemo pombe na sigara na ulaji wa nyama za mifugo inayofugwa,huku ikikuzwa kwa kuwekewa dawa ikiwemo kuku, ambavyo kwa pamoja huathiri mnyororo mzima. 

Alisema ipo haja kwa serikali kuangalia na kuona iwapo utafiti ufanyike ili kubaini hali ikoje nchini.

Kuhusu dawa ya Ujana alisema ni mojawapo ya dawa tano, zilizosajiliwa na Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala.

 Aliwataka waganga wa tiba asili na tiba mbadala, kutotangaza dawa za asili katika vyombo mbalimbali vya habari iwapo hazijasajiliwa. 

“Serikali inatambua tiba asili na mbadala lakini kumekuwepo na wimbi kubwa la waganga kutangaza dawa zao kinyume na utaratibu wa sheria huku wakijua kuwa mamlaka pekee ya usajili ni baraza ndio wenye kutoa ruhusa ya kitu gani kitangazwe,” alisema.

Aliongeza kuwa ni marufuku waganga kutoa matangazo bila kuwa na kibali kutoka baraza na kwamba matangazo yao, yanatakiwa kutambulisha wako wapi, mawasiliano na si dawa hiyo ina uwezo wa kutibu ugonjwa gani.

 Hata hivyo, Ndugulile alisema kumezuka wimbi la kuingizwa nchini mashine zikidai zina uwezo wa kutoa sumu na kupima magonjwa yote kwa wagonjwa, ambapo zinakuwa hazijapimwa na wala kutokuwa na vibali ikiwemo mashine ijulikanayo kama ‘Kwanta’. 

Alitoa agizo kwa Msajili wa Tiba Asili na Mbadala, kusaka mashine hizo na kuzikamata, ambapo msako ulifanyika kwa siku mbili Machi 6 na 7 mwaka huu. Akitaja dawa ambazo tayari zimesajiliwa na baraza hilo, Msajili Dk Ruth Suza alisema ni IH Myoon, Ujana, Coloidal Silver, Sudhi na Vatari.

IMEANDIKWA NA LUCY LYATUU - habarileo

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527