POLEPOLE ASHIRIKI UJENZI WA ZAHANATI YA KIJIJI CHA RUHURU KIGOMA

Katibu wa Itikadi na Uenezi CCM Humphrey Polepole ameshiriki zoezi la ujenzi wa zahanati ya kijiji cha Ruhuru Kata ya Muhange wilayani Kakonko mkoani Kigoma iliyoanza kujengwa na wananchi.


Aidha Polepole amewapongeza wananchi wa kijiji hicho kwa kujitolea kuanza ujenzi wa zahanati ya kijiji na kuahidi kuwa serikali italeta kiasi cha shilingi milioni 119 kwa ajili ya ujenzi wa Zahanati hiyo na kuhakikisha zahanati hiyo inakamilika kwa wakati.


Pongezi hizo alizitoa jana wakati wa ziara yake mkoani Kigoma ya kukagua utekelezaji wa ilani ya Chama Cha Mapinduzi na miradi ya maendeleo ambapo alijumuika na wananchi hao katika ujenzi wa zahanati hiyo na kuwahakikishia kuwa serikali itatoa kiasi hicho kwa ajili ya kumalizia ujenzi wa zahanati hiyo.


Polepole alisema serikali ya CCM imeamua kuongeza milioni 119 zitakazotumika kumaliza ujenzi na kuleta vifaaa tiba na wananchi waweze kupata huduma bora na waweze kufanya kazi kama kauli mbiu ya "Hapa Kazi tu" inavyosema na kutokana na juhudi hizo serikali itaendelea kushirikiana na wananchi na kuwapongeza kwa hatua hiyo.

"Niliona ni jambo zuri nije nishirikiane na nyie, nije mwenyewe tukutane kazini na mimi napenda kuwaambia habari njema kuwa serikali na viongozi wameona kazi nzuri mnayoifanya na tutahakikisha tunashirikiana kuhakikisha zahanati hii inakamilika na wananchi mnapata huduma bora za afya", alisema Polepole.

Diwani wa Kata ya Muhange Ibrahimu Katunzi alisema katika kijiji hicho kuna wakazi 2416 na wananchi walikuwa wanalazimika kutembea kilomita 16 kufuata huduma za afya katika vijiji vya Muhange na Kiduduye hali iliyowalazimu kuanzisha ujenzi wa zahanati ya kijiji ili kuweza kutatua changamoto hiyo.

Alisema wao kama uongozi walishirikiana na wananchi kufanya mkutano na kukubaliana kushirikiana kuchangia na kujitolea katika ujenzi wa nahanati na kuacha kusubiri kujengewa na serikali na baada ya kuanzisha ujenzi huo serikali imekubaliana kushirikiana nao na kutatua changamoto hiyo.


Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kakonko Kanali Hosea Ndagala aliwapongeza wananchi hao na kuendelea kuwahakikishia wananchi hao yakuwa serikali itaendelea kushirikiana nao na kuwaomba wananchi wa vijiji vingine kuunga mkono jitihada hizo kwa kuanzisha ujenzi wa zahanati kwa kuwa lengo la serikali ni kuhakikisha kila kijiji kinakuwa na zahanati.

Naye Mbunge wa viti maalumu mkoa wa Kigoma kupitia Vijana wa Chama cha Mapinduzi Zainabu Katimba aliwapongeza wananchi hao na kuwaomba wananchi waendelee kuiunga mkono serikali ya CCM ili waweze kupata miradi mingine zaidi kwa kuwa serikali ya CCM ni serikali inayotambua juhudi za wananchi na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na maendeleo.

Akiwa katika ziara yake Polepole pia alishiriki katika ufukiaji wa Mtaro wa maji katika kijiji cha Kanyomvi kata ya Kakonko na kuwahakikishia serikali itatoa fedha kwa ajili ya kumaliza changamoto zilizopo.

Na Rhoda Ezekiel- Malunde1 blog
Katibu wa Itikadi na Uenezi CCM Hamphrey Polepole ameshiriki zoezi la ujenzi wa zahanati ya kijiji cha Ruhuru Kata ya Muhange wilayani Kakonko mkoani Kigoma - Picha zote na Rhoda Ezekiel - Malunde1 blog 
Mbunge wa viti maalumu mkoa wa Kigoma kupitia Vijana wa Chama cha Mapinduzi Zainabu Katimba akishiriki ujenzi



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527