POLEPOLE ANG'OA 27 CHADEMA KAKONKO, ADAI MADIWANI WA CHADEMA KUFICHWA


Jumla ya wanachama 27 wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wamejiunga na Chama Cha Mapinduzi Wilayani Kakonko mkoani Kigoma katika kikao cha Halmashauri kuu ya Wilaya kilichoendeshwa na Katibu wa itikadi na uenezi CCM Humphrey Polepole.

Wakizungumza baada ya kukabidhiwa kadi na kiongozi huyo wananchi hao wamesema wamefikia uamuzi huo baada ya kuguswa na kazi nzuri inayofanywa na CCM na kukosa demokrasia Katika chama chao kutokana na Chama hicho kuwanufaisha watu wachache wenye vyeo.

Mmoja kati ya Wanachama wa CHADEMA waliohamia Chama Cha Mapinduzi,Liberatus Kamamba alieleza kuwa ameamua kuhamia katika chama hicho kutokana na utendaji kazi na utekelezwaji wa ilani ya chama hicho unavyofanywa na rais  Magufuli kuhakikisha fedha za serikali zinatumika ipasavyo.

Alisema mwanzoni viongozi walikuwa hawana utaratibu wa kuwatembelea wananchi na kuangalia changamoto wanazo kutananazo na kukagua miradi ya maendeleo lakini kwa sasa chama hicho kinafanya kazi hiyo na kuhakikisha kinawachukulia hatua wale wote wanaotumia fedha za serikali kwa matakwa yao binafsi na hivi sasa watumishi wote wanatembelea wananchi kutatua kero.

Naye Gidion Ruhaga alisema chama hicho kimerudisha heshima na utaratibu uliokuwepo na kinajali demokrasia na hakina ubaguzi.

Alisema chama alichokuwa akikitumikia kimekuwa kina ubaguzi na hakiwajali wanachama wanaopigana kukiweka madarakani na kwamba ni wa kwanza kuipinga serikali kuwa haitendi haki lakini hata wao hawafanyi hivyo na wamekuwa wa kwanza kujinufaisha na pesa zinazotolewa kwa ajili ya kukiendesha chama hicho.

Akizungumza na wanachama waliojitokeza katika kikao hicho,Polepole alisema amesikitishwa na kitendo kilicho fanywa na upinzani cha kuwafungia ndani madiwani wote wa chama hicho na kuwanyang'anya simu zao kwa kuhofia watahamia chama tawala.

Alisema viongozi hao baada ya kusikia kuwa kuna ugeni wa kiongozi huyo waliamua kuwaweka ndani madiwani na kusema kwamba kila mwananchi ana haki ya kuhamia chama chochote anacho kitaka hata wao wamewaachia viongozi na wanachama wengine kuhamia chama wanachokihitaji.

"Imeandikwa hata kwenye vitabu vya dini alaaniwe anae muogopa Mwanadamu nimeshangaa sana watu wanatuogopa hadi wanaamua kuwaficha madiwani wao, sisi hatutamnunua mtu kwa gharama yeyote ile hata huyo mbunge wenu akija kwetu hatumuhitaji tunahitaji wananchi wanaoamua wenyewe kujiunga na chama tawala kwa kuona utendaji kazi na misingi ya chama chetu", alisema Polepole.

Na Rhoda Ezekiel - Malunde1 blog
Katibu wa itikadi na uenezi CCM Humphrey Polepole akiwa katika kikao
Walioamua kuhamia CCM

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527