NEC YAWAJIBU LHRC WALIOANIKA DOSARI UCHAGUZI KINONDONI,SIHA....YADAI WAMEFANYA MAKOSA

Baada ya Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kutaja hadharani dosari kumi zilizojitokeza katika uchaguzi mdogo uliofanyika kwenye majimbo ya Kinondoni na Siha, Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Kailima Ramadhani amedai kuwa kituo hicho kimefanya makosa.


Alisema kituo hicho kimetangaza dosari hizo za uchaguzi uliofanyika Februari 17, bila kufuata sheria na kanuni za uchaguzi.


Uchaguzi huo ulifanyika baada ya waliokuwa wabunge wa majimbo hayo, Maulid Mtulia (CUF-Kinondoni) na Dk Godwin Mollel (Chadema-Siha) kujitoa kwenye vyama vyao na kuhamia CCM.


Wabunge hao wawili waliopitishwa tena kwenye uchaguzi huo kupitia CCM walishinda nafasi hizo.


Kutokana na uchaguzi huo, LHRC ilitoa dosari zilizofanana na zile zilizotolewa na vyama vya upinzani hasa Chadema.


Akizungumza wakati wa mahojiano na kituo cha Magic FM, Kailima alisema LHRC imefanya kosa la kisheria na kanuni kwa kutoa taarifa hiyo.


Alisema kifungu namba 4 cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi kimeielekeza tume hiyo kutunga kanuni wakati kifungu namba 64(4) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi kinasema Tume itatoa muongozo kwa watazamaji wa uchaguzi.


Alieleza kwamba hata katika uchaguzi wa mwaka 2015, tume hiyo ilitoa muongozo kwa watazamaji wa uchaguzi.


“Kipengele cha 12(d) kinasema mtazamaji hatatakiwa kutoa taarifa kwa umma juu ya mchakato wa uchaguzi hadi taarifa ya awali itakapokuwa imekabidhiwa na tume kukiri kupokewa kwa taarifa hiyo,” alisema Kailima.


Alifafanua kuwa kituo hicho kiliandika barua kwa tume na kuiwasilisha Februari 26 ambayo iliifikia tume Februari 28 jioni wakati ofisini kukiwa hakuna viongozi.


“Kutozingatia sheria ni kama wembe, utakukata tu,” alisema.


Mkurugenzi huyo alisema tume hiyo inatafakari iwapo itawapa kibali kingine cha utazamaji wa uchaguzi.


Kuhusu hoja zilizo kwenye taarifa hiyo ikiwamo ya matumizi ya watoto kwenye kampeni za chama kimojawapo, Kailima alisema wao si Wizara ya Afya, Jinsia, Wazee na Watoto na kwamba hoja hizo ilipaswa zipelekwe huko.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527