MHUDUMU AANGUKA KUTOKA KWENYE NDEGE

Mhudumu huyo alianguka kwenye mlango wa dharura wa ndege

Mhudumu wa ndege anadaiwa kujeruhiwa vibaya nchini Uganda baada ya kuanguka kutoka kwenye mlango wa dharura wa ndege ya shirika la Emirates.

Mwanamke huyo alikimbizwa hospitali akitokea uwanja wa ndege wa kimataifa wa Entebbe, karibu na mji mkuu Kampala,baada ya kuanguka mlangoni siku ya Jumatano.

Ndege aina ya Boeing 777 ilitua muda mfupi kabla, na ilikuwa ikijiandaa kupokea abiria kabla ya kuelekea Dubai.

Mazingira ya kuanguka kwake yanaendelea kuchunguzwa, huku kukiwa na ripoti za kukanganya kuhusu tukio hilo.

Hata hivyo, shirika hilo la ndege limethibitisha kutokea kwa ajali hiyo, likiiambia Gazeti la Khaleej Times.

''Tunaweza kuthibitisha kuwa mmoja wa wafanyakazi wetu bahati mbaya alianguka kwenye mlango uliokuwa wazi wakati alipokuwa akiiandaa ndege ili kupandisha abiria."

"Mfanyakazi huyo amepelekwa kwenye hospitali ya karibu. Tunatoa ushirikiano kadiri iwezekanavyo kwa mfanyakazi wetu, na kutoa ushirikiano zaidi kwa mamlaka zinazofanya uchunguzi.''
Chanzo-BBC

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527