MAMBOSASA: WAKIANDAMANA MITANDAONI HAKUNA TATIZO..BARABARANI WATAJUTA

Kamanda wa jeshi la polisi kanda maalum ya Dar es salaam Tanzania, Lazaro Mambosasa amefunguka na kusema kuwa kama April 26 mwaka huu watu wataandamana kwa mitandao ya kijamii wao hawana tatizo kwa hilo ila kama wataingia barabarani basi wasijute.

Mambosasa amesema hayo wakati akiongea na kituo cha habari cha kimataifa na kusema kuwa jeshi la polisi limejipanga kuwadhibiti watu ambao watataka kuvunja sheria za nchi kwa kuandamana barabarani. Mambo sasa amesema kuwa jeshi hilo limejipanga vizuri hivyo wanawakaribisha wale ambao watahamisika kuandamana barabarani. 

"Ndani ya kanda mimi nasema hakuna maandamano wanahamasishana wanapotezeana muda na wamezoea kufanya hivyo na walitishia kufanya hivyo wakati uliopita lakini tunachosema tumejipanga vizuri sisi ni wasimamizi wa sheria atakayetaka kuvunja sheria atapambana na sisi lakini asijutie matokeo ya kile atakachokutananacho, wakiandamana kupitia mitandao ya kijamii manake hakuna tutakaokutana nao barabarani hivyo wataandamana kwa kuendelea kupeana habari kwenye mitandao na hilo sisi hatuna shida ndio maana tunaendelea kupuuza yanayopangwa lakini yoyote atakayehamasika kupitia mtandao akaja barabarani kwa maana ya kuleta vurugu kuvunja sheria za nchi tutakutana naye tumejipanga" 

Mambosasa aliendelea kusema kuwa 

"Ulinzi upo tu unataka kujua kiasi gani tumejipanga kwa namna gani? Sisi tupo vizuri katika hilo na tunakukaribisha barabarani kama unataka kuandamana na wewe" alisisitiza Mambosasa 

Mange Kimambi amekuwa akihamasisha sana watu kupitia mitandao ya kijamii kuandamana katika siku ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ambapo kila mwaka sherehe hizo huwa zinafanyika tarehe 26 mwezi wa nne.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527