JOKATE MWEGELO ATUMBULIWA UVCCM



Kamati ya Utekelezaji ya Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi(UVCCM), imetengua uteuzi wa nafasi ya Kaimu Katibu wa Idara ya Uhamasishaji na Chipukizi wa Umoja huo iliyokuwa ikiongozwa na Jokate Mwegelo.

Jokate aliteuliwa Aprili mwaka jana na Kamati hiyo kukaimu kwa muda kabla ya kamati hiyo kufanya uchaguzi.

Kaimu Katibu Mkuu Taifa wa Umoja Shaka Hamdu amekiri Jokate kutenguliwa kwa nafasi hiyo leo Machi 25, 2018 kupitia vikao vya Kamati vilivyokutana kwa mujibu wa kanuni na taratibu za UVCCM.

“Kwanza ifahamike Jokate aliteuliwa kukaimu kwa utaratibu wa UVCCM na ameondolewa kwa utaratibu, ni kama alikuwa kwenye majaribio,” amesema Shaka.


Shaka amesema utaratibu wa kujaza nafasi hiyo utafanyika hapo baadaye kupitia vikao vya umoja huo.

Uteuzi wa Jokate kuwa Kaimu Katibu wa Idara ya Uhamasishaji na Chipkizi, ulionekana kutaka kuivuruga jumuiya hiyo baada ya kuibuka mjadala kwa viongozi na wanachama wakidai uteuzi huo haukufuata kanuni na taratibu za umoja huo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527