MCHINJA MBUZI AJIUA MACHINJIONI SHINYANGA


Askari wa Jeshi la Polisi mkoa wa Shinyanga wakiutoa mwili wa marehemu Wandiba John kwenye choo cha machinjio ya mbuzi Ndembezi katika manispaa ya Shinyanga mahali ambapo amejinyonga kwa madai ya kukabiliwa na ugumu wa maisha huku wananchi na wachinja mbuzi wenzake wakishuhudia tukio hilo.
Baadhi ya wachinja mbuzi wa eneo la Kata ya Ndembezi Manispaa ya Shinyanga, wakiwa wamesitisha shughuli zao za uchinjaji mbuzi, mara baada ya mwezao kujinyonga na kufariki dunia majira ya saa 10 alifajiri usiku wa kuamkia leo.
***

Kijana aliyefahamika kwa jina la Wandiba John (26), mkazi wa Kata ya Ndembezi Manispaa ya Shinyanga amefariki dunia kwa kujinyonga katika eneo lake la kufanyia kazi kwenye machinjio ya mbuzi ya kata hiyo kwa kile kilichodaiwa kuwa maisha ni magumu.

Tukio hilo limetokea leo alfajiri Februari 26,2018 kwenye machinjio hayo ya mbuzi kata ya Ndembezi manispaa ya Shinyanga ambapo marehemu huyo amekutwa na wenzake akiwa amejinyonga kwenye korido la choo cha machinjio hayo na hivyo kusababisha shughuli za uchinjaji mbuzi kusitishwa.

Wachinja mbuzi wa eneo hilo  walisema walipofika kufanya shughuli zao za uchinjanji mbuzi kama kawaida yao majira ya saa 11 alfajiri ndipo wakaona mwili wa mwenzao ukiwa umening'inia juu ya choo cha machinjio hayo na ndipo walipotoa taarifa polisi ambao walifika na kuuchukua mwili huo.

“Huyu marehemu kwao kabisa ni Musoma na huku alikuja kutafuta maisha, na alikuwa akikaa ghetto hapa Ndembezi, na alikuwa mywaji sana wa pombe aina ya gongo na kila siku alikuwa akisema ipo siku atawatia hasara familia yake kwani maisha ni magumu, na hatimaye amekamilisha usemi wake,”alisema mmoja wa wachinjaji hao Dankani Buti.

Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani Shinyanga Kamishina msaidizi wa Polisi ACP Simon Haule alithibitisha kutokea kwa tukio hilo, na kubainisha kuwa mwili huo wa marehemu umepelekwa kwenye chumba cha kuhifadhia maiti katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Shinyanga.

Naye Mganga mfawidhi wa hospitali hiyo ya rufaa ya mkoa wa Shinyanga George Masigati alisema waliupokea mwili huo wa marehemu majira ya saa 11 asubuhi na kubainisha kuwa tayari umehifadhiwa kwenye chumba cha maiti wakisubiri ndugu zake kuuchukua kwenda kuuhifadhi kwenye makazi yake ya milele. 

HABARI KWA HISANI YA SHINYANGANEWS BLOG

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527