HII HIZI HAPA BEI ELEKEZI ZA MAFUTA AINA YA PETROLI KUANZIA FEBRUARI 7 KOTE NCHINI

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (Ewura) imetangaza bei mpya za mafuta zinazoanza kutumika leo Februari 7, 2018 huku bei za petroli, dizeli na mafuta ya taa zikipanda.

Taarifa kwa umma iliyotolewa leo na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Ewura, Nzinyangwa Mchany imesema bei za rejareja zimeongezeka kwa petroli ikiwa ni Sh59 sawa na asilimia 2.70, dizeli Sh46 (sawa na asilimia 2.30), na mafuta ya taa kwa Sh24 (sawa na asilimia 1.17).

Amesema bei za jumla nazo zimeongezeka ambazo kwa petroli ni Sh58.57 sawa na asilimia 2.85, dizeli kwa Sh46.48 (sawa na asilimia 2.44) na mafuta ya taa kwa Sh23.75 (sawa na asilimia 1.24).

Mchany amesema ongezeko hilo linatokana na bei kuongezeka katika soko la dunia.

“Bei za jumla na rejareja kwa mafuta ya petroli na dizeli yaliyoingizwa nchini kupitia Bandari ya Tanga nazo zimeongezeka ikilinganishwa na toleo lililopita la Januari 3. Bei za mafuta ya taa hazijabadilika kwa sababu hakuna yaliyoingizwa nchini kupitia bandari hiyo Januari,” amesema Mchany.

Amesema bei za rejareja katika mikoa ya Kaskazini zimeongezeka, ambazo petroli ni kwa Sh15 sawa na asilimia 0.70 na dizeli kwa Sh47 sawa na asilimia 2.29. Bei za jumla zimeongezeka petroli ikiwa ni kwa Sh15.36 sawa na asilimia 0.73 na dizeli Sh47.18 sawa na asilimia2.42.

“Ongezeko la bei za mafuta ya petroli na dizeli katika Mkoa wa Tanga linatokana na mabadiliko ya bei za mafuta katika soko la dunia na kuongezeka kwa gharama za usafirishaji,” amesema Mchany.

Kaimu mkurugenzi mkuu huyo amesema sehemu ya shehena kubwa ya mafuta yaliyopokewa katika Bandari ya Dar es Salaam ni yenye bei ya soko la dunia za Novemba, 2017 wakati iliyopokewa katika Bandari ya Tanga ni ya bei ya soko la dunia ya Desemba 2017.

Amesema bei za mafuta katika soko la dunia kwa Novemba 2017 ziko juu kwa zaidi ya asilimia sita ikilinganishwa na bei za Oktoba 2017, wakati bei za Desemba zina mabadiliko tofauti.

Amesema bei ya petroli imepungua kwa asilimia 0.2 na ya dizeli na mafuta ya taa imeongezeka kwa asilimia 2.7 na asilimia 1.9.

“Kampuni za mafuta ziko huru kuuza bidhaa za mafuta ya petroli kwa bei ya ushindani ili mradi tu bei hizo zisivuke  bei kikomo kama ilivyokokotolewa na kanuni iliyopitishwa na Ewura,” amesema Mchany.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527