ZOEZI LA UPIGAJI CHAPA MIFUGO LAONGEZEWA MUDA WA MWEZI MMOJA

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina ameongeza muda wa mwezi mmoja kwa Halmashauri hapa nchini kukamilisha zoezi la upigaji chapa mifugo na kuwataka watendaji wote wa Serikali wanaohusika kuhakikisha mifugo yote inapigwa chapa. 


Waziri Mpina ameyasema hayo wakati wa kuhitimisha zoezi la upigaji chapa Kitaifa katika Kijiji cha Migato wilaya ya Itilima mkoani Simiyu, zoezi ambalo lilianza rasmi Kitaifa mwezi Desemba, 2016 na kupangwa kukamilika Desemba 31, 2017. 


“Kwa kuwa hadi sasa zoezi hili limetekelezwa kwa asilimia 38.5 kutokana na sababu mbalimbali, Mimi Luhaga Mpina Waziri wa Mifugo na Uvuvi kwa Mamlaka niliyopewa chini ya sheria ya Utambuzi, Usajili na ufuatiliaji wa mifugo ya mwaka 2010 na kanuni yake, ninaongeza muda wa kupiga chapa mifugo kutoka tarehe 01/01/ 2018 hadi 31/01/2018”alisititiza. 


Mpina amesema miongoni mwa changamoto zilizopelekea Halmashauri nyingi kushindwa kutekeleza zoezi hilo kwa asilimia 100 ni baadhi ya halmashauri kutokutenga fedha kwa ajili ya zoezi hilo, kubaini mifugo kutoka nje ya nchi, baadhi ya wafugaji kushindwa kutaja idadi halisi ya mifugo yao na baadhi ya Halmashauri kuwatoza wafugaji zaidi ya shilingi 500 ambayo ndiyo bei elekezi, ambapo ameagiza wafugaji hao waliotozwa zaidi ya shilingi 500 warejeshewe fedha zao. 

Ameongeza kuwa hadi kufikia Desemba 31, 2017 Halmashauri 30 hapa nchini hazijapiga kabisa chapa mifugo, halmashauri 23 zimeendesha zoezi hilo chini ya asilimia 10 na akaongeza kuwa orodha ya majina ya viongozi wa wilaya hizo walioshindwa kutekeleza agizo hilo la Serikali ameyawasilisha kwa Waziri Mkuu wa Tanzania Mhe.Kassim Majaliwa. 

“Halmashauri 30 ambazo hazijapiga chapa kabisa hata ng’ombe mmoja na zile 23 ambazo zimepiga chini ya asilimia 10 majina ya viongozi wote na Halmashauri husika nimekabidhi orodha hiyo kwa Waziri Mkuu, hatuwezi kuendekeza ukaidi wa maagizo ya Viongozi Wakuu wa Nchi” alisema Mpina. 

Akiwasilisha taarifa ya zoezi la Upigaji Chapa katika Mkoa wa Simiyu, Mwakilishi wa Katibu Tawala Mkoa, Ndg.Elias Kasuka amesema zoezi hilo mkoani humo lilianza rasmi mwezi Aprili 2017 ambapo hadi sasa ng’ombe zaidi ya 764, 933 wameshapigwa chapa kati ya ng’ombe 1,500,000. 

Akitoa maoni yake baada ya kuhitimisha zoezi la upigaji chapa mifugo, Paulo Mabula mfugaji kutoka Migato Itilima amesema wafugaji wamelipokea kwa furaha agizo la Waziri wa Mifugo na Uvuvi kuongeza siku za kwa ajili ya kupiga chapa kwani litawasaidia wafugaji ambao bado hawajakamilisha ili kuondokana na changamoto ya wizi wa mifugo. 

Naye Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Itilima, Mhe.Mahamoud Mabula amemuomba Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe.Luhaga Mpina kuwasaidia wafugaji wa Wilaya hiyo na maeneo mengine ya Mkoa huo kufanya vikao vya ujirani mwema na wale wa mikoa jirani ili kujadiliana namna ya kuondoa changamoto ya wizi wa mifugo. 

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Itilima Mhe.Benson Kilangi amesema viongozi na wataalam wa wilaya hiyo wamekuwa wakiwahamasisha wafugaji kupanga matumizi bora ya ardhi ili waweze kutenga maeneo kwa ajili ya malisho na kuyawekea miundombinu muhimu kwa ajili ya mifugo ikiwemo maji, majosho pamoja malisho.

Na Stella Kalinga, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu
Vijana wa Skauti wilaya ya Itilima wakimvisha skafu Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina alipowasili wilayani humo kwa ajili ya kuhitimisha zoezi la upigaji chapa mifugo kitaifa, mkoani Simiyu.
Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina akisalimiana na Afisa Mifugo kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Ndg.Ally Mzee mara baada ya kuwasili mkoani humo kwa ajili ya kuhitimisha zoezi la upigaji chapa mifugo Kitaifa, lililofanyika katika kijiji cha Migato wilayani Itilima.
Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina akisalimiana na Mwakilishi wa Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Ndg.Elias Kasuka mara baada ya kuwasili Mkoani humo kwa ajili ya kuhitimisha zoezi la upigaji chapa mifugo Kitaifa, lililofanyika katika kijiji cha Migato wilayani Itilima.
Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina akipokelewa na Viongozi wa Wilaya ya Itilima mkoani Simiyu mara baada ya kuwasili wilayani humo kwa ajili ya kuhitimisha zoezi la upigaji chapa mifugo Kitaifa, lililofanyika katika kijiji cha Migato wilayani Itilima.
Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina(wa pili kushoto) akipiga chapa ng’ombe katika hitimisho la zoezi la upigaji chapa mifugo Kitaifa katika Kijiji cha Migato, Wilaya ya Itilima Mkoani Simiyu.
Mkuu wa Wilaya ya Itilima, Mhe.Benson Kilangi (wa tatu kushoto) akipiga chapa ng’ombe katika hitimisho la zoezi la upigaji chapa mifugo Kitaifa katika Kijiji cha Migato, Wilaya ya Itilima Mkoani Simiyu ambalo limehitimishwa na Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Itilima, Daudi Nyalamu akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Migato na vijiji jirani mara baada ya Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina kuhitimisha zoezi la upigaji chapa mifugo Kitaifa lililofanyika kijijini hapo.
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe.Luhaga Mpina akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Migato na vijiji jirani mara baada ya kuhitimisha zoezi la upigaji chapa mifugo Kitaifa lililofanyika kijijini hapo.
Mbunge wa Jimbo la Itilima, Mhe.Njalu Silanga akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Migato na vijiji jirani mara baada ya Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina kuhitimisha zoezi la upigaji chapa mifugo Kitaifa lililofanyika kijijini hapo.
Ndg.Paulo Mabula akitoa mchango wake mara baada ya Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina kuhitimisha zoezi la upigaji chapa Kitaifa katika Kijiji cha Migato wilaya ya Itilima Mkoani Simiyu
Picha na Stella Kalinga, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527