WAZIRI MKUU KASSIM MAJALIWA KESHO KUFANYA MKUTANO NA WADAU WA PAMBA SHINYANGA


Waziri mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa kesho Ijumaa Disemba 22,2017 atafanya mkutano na wadau wa pamba kutoka mikoa 16 nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Zainab Telack (pichani) amesema mkutano huo utakaokutanisha pamoja wadau wa pamba utafanyika katika shule ya sekondari Savannah iliyopo katika eneo la Ibadakuli manispaa ya Shinyanga.

“Mkutano huu utahudhuriwa na watu zaidi ya 1,000 wakiwemo mawaziri,wabunge, watendaji wakuu kutoka ngazi ya wizara,mikoa,wilaya,taasisi ,mashirika ya umma na wadau mbalimbali”,alieleza Telack.

“Serikali imedhamiria kuhakikisha kuwa wananchi wanalima zao la pamba kwa wingi na kulifanya zao hilo lililokuwa limedorora sasa linakuwa na tija na kuwanufaisha wakulima hivyo mkutano huu utakuwa na majibu kwa wakulima na wadau wote”,aliongeza Telack.

Mkuu huyo wa mkoa alisema waziri mkuu pia atatembelea kiwanda cha Nyuzi kilichopo katika kata ya Kizumbi katika manispaa ya Shinyanga.

Aidha alisema pia kutakuwa na maonesho ya biashara na shughuli mbalimbali zinazofanyika mkoani Shinyanga.

Telack alisema katika msimu huu wa kilimo cha pamba zaidi ya wakazi 80,000 wanatarajiwa kulima zao la pamba na wamepanga kulima katika ekari 67,579.9.
Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Zainab Telack akizungumza na waandishi wa habari leo wakati akitoa taarifa kuhusu ujio wa Waziri mkuu Kassim Majaliwa mkoani Shinyanga
Waaandishi wa habari wakichukua matukio wakati wa kikao hicho.
Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527