SAKATA LA AIRTEL LAZIDI KUKOLEA....TEWUTA NAO WAIBUKA

Chama cha Wafanyakazi wa Sekta ya Huduma za Mtandao wa Mawasiliano Tanzania (Tewuta) kimepongeza hatua ya Rais John Magufuli kumtaka Waziri wa Fedha kuanza uchunguzi kubaini ukweli kuhusu ubinafsishwaji wa Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL).


Katibu Mkuu wa Tewuta, Junus Ndaro amesema chama hicho kinatambua fika kuwepo mchezo mchafu uliosababishwa na Watanzania wachache wenye uchu wa fedha wakisaidiana na wawekezaji kupora rasilimali hiyo ya Taifa.


Ndaro amesema leo Alhamisi Desemba 28,2017 kuwa, kwa muda mrefu chama hicho kimekuwa kikitoa malalamiko kuhusu ufisadi huo serikalini lakini hakikusikilizwa.


“Tunampongeza Rais Magufuli kwa kuthubutu kutamka pasipo shaka kuwa taarifa alizonazo zinaonyesha kampuni ya Airtel ni mali ya TTCL, jambo hili tulilipigia kelele kwa muda mrefu,” amesema.


Ndaro amesema mara zote hawakusita kutamka kuwa Celtel ambayo sasa ni Airtel ni mali ya TTCL iliyoporwa pasipo kulipwa chochote.


“Wafanyakazi tunatambua kuwa TTCL haikuporwa Celtel pekee bali ilinyang’anywa pia Chuo cha Posta na Simu hali iliyosababisha tukose mahali pa kupata mafunzo,” amesema Ndaro.


Kutokana na kuanza uchunguzi wa sakata hilo, Ndaro amesema viongozi wa Tewuta wako tayari kutoa kila aina ya ushirikiano kuhakikisha Serikali inashinda na kuirudisha Airtel mikononi mwa TTCL.


“Tuna ushahidi wa kutosha na tuko tayari kutoa ushirikiano kwa Serikali katika hatua zote kuleta haki iliyopotea ya Kampuni ya Simu Tanzania,” amesema.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527