Picha : DC SHINYANGA AKABIDHI ZAWADI ZA SIKUKUU YA MWAKA MPYA 2018 ZA UMWABU KWA WATOTO WENYE UALBINO BUHANGIJA


Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro ametoa wito kwa wananchi wa mkoa wa Shinyanga kujenga utamaduni wa kusaidia watu wenye uhitaji kwa kuwatatulia changamoto zinazowakabili ili kujiwekea thawabu kwa mwenyezi Mungu na siyo kuwatenga.


Matiro ametoa rai hiyo leo Desemba 30,2017 kwenye kituo cha kulelea watoto wenye ualbino cha Buhangija mjini Shinyanga wakati akikabidhi zawadi ya chakula kwa watoto hao kwa ajili ya kusheherekea sikukuu ya kuukaribisha mwaka mpya 2018, vyakula vilivyotolewa na kikundi cha Umwabu kilichopo mtaa wa Busulwa Kata ya Kitangili manispaa ya Shinyanga.

Alisema wakazi wa Shinyanga wanatakiwa kubadilika kwa kila mmoja kuguswa na hitaji la mwenzake ,na huo ndiyo upendo na siyo kuwatenga kwani mtu ambaye anamsaidia mwenzake anajiwekea faida kwa mwenyezi Mungu pamoja na kupata baraka.

“Nimefanya utafiti (Research) nimegundua idadi kubwa ya wananchi wa Shinyanga wanakabiliwa na maisha magumu juzi juzi nimetoa msaada katika Kata ya kitangili nimekutana na watu zaidi ya 200 wanaishi maisha ya shida, hivyo naomba wana Shinyanga tusaidiane sisi kwa sisi tusingoje watu kutoka nje,”alisema Matiro.

Aliongeza kuwa kama mtu ana nguo nyingi asizitupe ampatie yule ambaye hana au kama ana chakula amgawie na mwenzake na siyo kukitupa jalalani na huo ndiyo upendo ambao tunautaka tuishi kwa kusaidiana na siyo kunyoosheana vidole.

Hata hivyo Matiro alikipongeza Kikundi cha Umwabu kwa kuguswa na watoto hao wenye ualbino kwa kuchangishana fedha na kuwapatia zawadi ya chakula cha sikukuu ya mwaka mpya na kuvitaka vikundi vingine viige mfano huo kwa kuwa na uzalendo wa kusaidiana.

Naye mwenyekiti wa kikundi hicho Jeremiah Alango alisema wao kama wanakikundi moja ya falsafa yao ni kusaidiana kwenye shida na raha pamoja na kutoa misaada kwa watu wenye uhitaji na ndiyo sababu iliyowagusa kusaidia watoto hao wenye ualbino chakula hicho cha Sikukuu ya Mwaka mpya.

Alivitaja vyakula walivyotoa kuwa ni mchele kilo 50, mbuzi wawili, sukari kilo 25, unga wa ngano kilo 25, mafuta ya kupikia lita 10, chumvi katoni moja, maharage kilo 20, soda katoni saba, sabuni za unga mifuko miwili, sabuni za mche boksi 4, Mpoa na b lash za kufanyia usafi 18,pamoja na majani ya chai dazani moja.

Kwa upande wake mlezi wa kituo hicho Mwalimu Suleimani Kipanya akizungumza kwa niaba ya watoto hao Albino, alishukuru kwa zawadi hiyo ya chakula na kusema kimekuja muda muafaka ambapo watoto hao watakula na kunywa na kujiona jamii inayowazunguka ipo pamoja nao na kusheherekea sikukuu hiyo kwa furaha.
Na Marco Maduhu - Malunde1 blog
ANGALIA PICHA HAPA CHINI
Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akizungumza katika kituo cha watoto wenye ualbino cha Buhangija ambapo alitoa wito kwa wananchi wa mkoa wa Shinyanga kujenga tabia ya kusaidiana kutatua changamoto kwa watu wenye uhitaji- Picha na Marco Maduhu - Malunde1 blog
Mwenyekiti wa Kikundi cha Umwabu cha Mtaa wa Busulwa Kata ya Kitangili Jeremiah Alango akizungumza ambapo alisema moja ya falfasa katika kikundi chao ni kusaidiana kwenye shida na raha pamoja na kutoa msaada kwa watu wenye uhitaji na ndiyo maana wameguswa na kuamua kutoa zawadi hiyo ya chakula kwa watoto hao wenye ualbino.
Katibu wa Kikundi cha Umwabu Mweya Wambura akisoma risala ya Kikundi kuwa kilianzishwa Mwaka  2016 na umoja wa majirani waishio mtaa huo wa Busulwa wakiwa watu 19, na hadi sasa wapo 87, na dhumuni lake ni kusaidiana kwenye shida na raha ,kusaidia makundi maalumu, ambapo kimeshasajiliwa na serikali kwa utambulisho namba SMC 778 ambapo pia kitashirikiana na serikali kusukuma gurudumu la maendeleo.

Watoto wakisikiliza maneno kutoka kwa viongozi wa kikundi cha Umwabu

Baadhi ya zawadi zikiwa eneo la tukio

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine akiangalia zawadi hizo

Mkuu wa wilaya Josephine Matiro akigawa soda za kopo kwa watoto hao wenye ualbino
Mkuu wa wilaya Josephine Matiro akiwa na wanakikundi cha Umwabu wakigawa soda za kopo kwa watoto hao wenye ualbino

Msimamizi wa kituo cha Buhangija Seleman Kipanya akiwa amebeba soda kwa ajili ya kuzigawa kwa watoto

Watoto wakiwa na soda zao

Watoto wakiwa wameshikilia soda

Mbuzi wa sikukuu ya mwaka mpya wakiwa wamefungwa kamba kabla ya kukabidhiwa kwa watoto
Mwenyekiti wa kikundi cha Umwabu Jeremiah Alango akikabidhi mbuzi wa kitoweo cha siku ya sikukuu ya Mwaka mpya 2018 kwa watoto wanaolelewa katika kituo cha Buhangija
Zoezi la kukabidhi zawadi za mwaka mpya likiendelea
Baadhi wa wanakikundi cha Umwabu wakiwa eneo la tukio kukabidhi zawadi ya chakula kwa watoto  wenye ualbino
Picha na Marco Maduhu - Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527