MUME AUA MKE KWA KUMCHOMA KISU KUTOKANA NA WIVU WA MAPENZI


Mkazi wa barabara ya Sikonge mkoani Tabora, Kapezi Fundikira (28) ameuawa kwa kuchomwa kisu na mume wake kutokana na wivu wa mapenzi. 

Kamanda wa Polisi, Mkoa wa Tabora, Wilbroad Mutafungwa alisema tukio hilo ni la Desemba 26, mwaka huu asubuhi katika eneo la barabara ya Sikonge.

Kwamba chanzo cha mauaji hayo ni wivu wa mapenzi. Alimtaja mume wa Kapezi kuwa ni Issa Hamisi na kwamba baada ya kutenda mauaji hayo, alikimbia na juhudi za jeshi la polisi za kumtafuta zinaendelea.

Alisema polisi inaendelea kufanya doria usiku na mchana katika maeneo yote katika manispaa ya Tabora ili kuuweka mji vizuri na kudhibiti matukio ya mauaji na wizi usiku.

 Mutafungwa alisema polisi mkoani Tabora inawaomba wananchi kutoa ushirikiano ili mtuhumiwa akamatwe na afikishwe mahakamani.

Wakati huo huo kijana mmoja, Michael Peter (20), mkazi wa Kata ya Chem Chem amegundulika amekufa akiwa ndani ya kilabu cha pombe za kienyeji.

 Kamanda Mutafungwa alisema tukio hilo ni la Desemba 26, mwaka huu, majira ya saa 11 jioni maeneo ya mtaa wa Masempele Kata ya Ngambo, Manispaa ya Tabora.

Alisema Peter alikunywa pombe za kienyeji kupita kiasi na kusababisha kifo chake. Kwamba mwili wake baada ya uchunguzi, ulikabidhiwa kwa ndugu kwa ajili ya mazishi

IMEANDIKWA NA LUCAS RAPHAEL - habarileoTABORA

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527