MBINU YA KUOMBA PENZI KWA KUPAPASA MIGUU YA WANAWAKE YAWAPONZA WANAUME SINGIDA



MILA inayoendelea na jamii ya Ihanja Wilaya ya Ikungi mkoani Singida ya wanandoa kuishi nyumba tofauti, inachangia wanaume kunyanyaswa kijinsia kwa kunyimwa haki ya tendo la ndoa.


Mila hiyo ni kwamba, mume anakuwa na nyumba yake na anaishi na watoto wa kiume. Mke naye anakuwa na nyumba yake na anaishi na watoto wa kike.

Mbinu inayofanyika kumtoa mke ili wakapeane haki ya tendo la ndoa, mume akiingia anakolala mke wake na watoto wake wa kike, humpapasa miguuni.

Kwa vile mke anajua akipapaswa miguuni ni kwamba anaombwa tendo la ndoa, mke huamka na kwenda mahali walikokubaliana kufanya tendo hilo muhimu kwa ustawi wa ndoa.

Hayo yamesemwa juzi na kundi la wanaume kwenye mkutano wa hadhara ulioitishwa na shirika lisilo la kiserikali  la Save the Mother and Children of Central Tanzania (SMCCT). Lengo la mkutano huo, ni kutoa elimu kwa jamii juu ya madhara ya ukatili wa kijinsia na ukeketaji.

Ofisa Mtendaji Kata ya Ihanja, Hamisi Mpuma, amesema ofisi yake imekuwa ikipokea mara kwa mara malalamiko/migogoro ya kifamilia, ambayo chanzo chake kikuu ni ukatili wa kijinsia wa kunyimana tendo la ndoa.

Akifafanua, alisema baadhi ya wanawake kwa sababu wanazozijua wao, wamekuwa wakitumia mwanya wa kulala na watoto wa kike, kuwanyima tendo la ndoa wanaume zao.

“Wakifuatwa na waume zao usiku, wanadai watoto wa kike bado hawajazidiwa na usingizi, hivyo tendo la ndoa halitafanyika. Hali hiyo haitokei mara moja, inajirudia kwa siku tofauti tofauti. 

Unyanyasaji huo, husababisha mwanamume kuhamishia hasira kwa watoto. Mtoto akimwomba kitu baba yake, baba yake humjibu kwa ukali, nenda kamwambie mama yako,” alifafanua.

Kuhusu mbinu ya kupapasa mke miguu usiku, alisema hivi karibuni aliletewa malalamiko na binti mmoja (hakumtaja) akimlalamikia baba yake kumpapasa miguu usiku wakati wamelala.

“Baada ya kumwita baba huyo anayelalamikiwa na binti yake, alijitetea kwamba hakuwa na nia mbaya kwa binti yake, isipokuwa alikuwa anataka kumwamsha mke wake ili wakafanye tendo la ndoa. Baada ya utetezi huo, tulimwomba binti amsamehe baba yake, kwa vile hakuwa na nia mbaya,” alisema.

Akichangia hoja hiyo, Joseph Msukuya, alisema wakati umefika jamii ya Ihanja kubadilika na kuwa na nyumba/chumba kimoja kwa ajili ya mume na mke tu.

“Tuachane na hii mila, kwanza imeshapitwa na wakati na haipendezi mume unatoka usiku wa manane kwenda kupapasa mguu wa mke wake katikati ya miguu ya watoto wa kike. Wanaume kuweni na chumba kimoja cha kulala na kufanya mambo yenu ya kupeana haki ya tendo la ndoa,” amesisitiza Msukuya.
Na Nathaniel Limu -Singida

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527