WAGOMBEA CCM MIKOA NAO KUISOMA NAMBA



Halmashauri Kuu ya CCM inakutana jijini Dar es Salaam katika kikao ambacho pamoja na mambo mengine itapitia na kufanya uteuzi wa majina ya wanachama walioomba uongozi kwenye chama na jumuiya zake ngazi ya mkoa na Taifa.
Katibu wa Itikadi na Uenezi, Humphrey Polepole alisema kikao hicho kinachokutana baada ya Kamati Kuu kukamilisha kikao chake jana, mbali na kujadili wagombea kinakusudia kupokea tathimini ya uchaguzi mdogo wa udiwani unaotarajiwa kufanyika katika kata 43 Jumapili ijayo.
Tofauti na vikao vilivyopita vilivyofanyika bila kuwapo Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana kwa kilichoelezwa kuwa alikuwa na matatizo ya kifamilia, safari hii ameonekana kwenye picha za kikao cha Kamati Kuu jana.
Mara ya mwisho kikao hicho kiliketi Septemba 27 kwa ajili ya kufanya kazi kama hiyo katika ngazi ya wilaya, ikiwa ni mwendelezo wa mchakato wa uchaguzi wa ndani wa chama hicho, unaoelezwa kuwa baadhi ya wagombea “wanaisoma namba” baada ya majina yao kuchujwa.
Kama ilivyokuwa wakati uchaguzi wa wilaya na matawi na mashina, wagombea watakaopitishwa watakuwa na wakati mgumu kujua mustakabali wao hadi watakapotangazwa mbele ya mkutano wa uchaguzi, ikiwa ni staili mpya chama hicho inayozuia kujitangaza wala kujinadi.
Staili hiyo ya uchaguzi ambayo ni ngeni ndani ya chama hicho, inaweza kuwaangusha wagombea wengi au kubatilisha chaguzi kwa watakaokwenda kwa mazoea ya miaka mingi ya kutegemea fedha na umaarufu kama mtaji wao.
Katika hatua ya wilaya chama hicho kilifuta chaguzi katika wilaya sita na safari hii wagombea wa wilaya hiyo wameteuliwa na kamati juu iliyokutana juzi.
Pia chaguzi katika kata 44 zilibatilishwa kutokana na kubainika mambo yaliyopigwa marufuku kama kuwa na makundi, kupanga safu na kuweka mapandikizi au wasaliti.
Mambo mengine yaliyojitokeza katika ngazi za awali ambayo yanaweza pia kujitokea ngazi ya mikoa ni kupitisha wagombea ambao ni watuhumiwa wa ubadhirifu wa mali za chama; wasio wakazi wa maeneo husika; waliopitishwa baada ya wengine kuonewa katika uteuzi na kuwapo mgombea mmoja tu aliyepitishwa.
Vilevile lilikuwapo tatizo la kutolewa taarifa zisizo sahihi kuhusu wagombea zenye lengo la kupotosha vikao vya juu.
Walioteuliwa
Wilaya ya Hai
Abdullah Mriri
Magai Maganda
Justice Masawe
Wilaya ya Siha
Justice Mkita
Wlfred Mossi
Humfrey Nnko
Wilaya ya Makete
Aida Chengula
Mwawite Njajilo
Onna Nkwama
Wilaya ya Musoma Mjini
Robert Sylivester
Magiri Maregesi
Amina Nyamgambwa
Daudi Misango
Wilaya ya Musoma vijijini
Gerald Kasonyi
Kananda Kananda
Nyabukika Nyabukika.     
Imeandikwa na Tausi Mbowe, Mwananchi 

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527