POLISI WADAI KUUA WATU WATANO WANAODHANIWA KUWA NI MAJAMBAZI KAHAMA


Watu watano wanaosadikiwa kuwa majambazi wameuawa kwa kupigwa risasi na polisi waliokuwa doria.


Taarifa ya polisi imesema watu hao waliuawa walipojaribu kuwavamia wafanyabiashara wa madini katika machimbo ya Mwime nje kidogo ya Mji wa Kahama.

Watuhumiwa pia wanadaiwa kuhusika na mauaji ya viongozi wa Serikali ya Mtaa, polisi na wanasiasa mkoani Pwani katika wilaya za Kibiti, Rufiji na Mkuranga.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Simon Haule alisema jana kwamba watu hao walijeruhiwa usiku wa kuamkia jana katika eneo la Mwanva katika Halmashauri ya Mji wa Kahama walipokabiliana ana kwa ana na polisi waliofika eneo hilo.

Kamanda Haule alisema baada ya polisi kufika kwenye eneo la tukio, watu hao walijificha kwenye mashimo yanayotumiwa kuchimba mchanga na kuanza kurushiana risasi na askari.

Alisema katika mapambano hayo, watuhumiwa walizidiwa nguvu na kujeruhiwa na walifariki dunia walipokuwa njiani kupelekwa hospitali.

Alisema katika eneo la tukio, polisi walikuta bunduki moja aina ya SMG na risasi 25 zilizokuwa kwenye magazini. Pia walikuta mabomu mawili ya kutupa kwa mkono.

Katika uchunguzi wa awali, Kamanda Haule alidai kwamba watu hao ni miongoni mwa waliokuwa wakifanya uhalifu mkoani Pwani ambao walikimbia huko baada ya kudhibitiwa.

Kamanda Haule aliwataka wananchi kufika katika Hospitali ya Mji wa Kahama kuwatambua marehemu kauli ambayo pia ilitolewa na Mganga Mkuu wa Mji wa Kahama, Dk David Lucas.

Shuhuda wa tukio hilo, Justina Elias alisema walisikia milio ya risasi saa tatu usiku wa kuamkia juzi na baada ya muda walitoka kwenda kuangalia na kukuta watu wakiwa wameuawa.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527