ALIYEJIFANYA MWANDISHI WA HABARI NA KUTAPELI WAANDISHI WA HABARI ATUPWA JELA SHINYANGA


Kijana huyo akiwa chini ya ulinzi wa polisi

Mahakama ya mwanzo ya wilaya ya Kahama mkoa wa Shinyanga imemhukumu kwenda jela miezi minne au kulipa faini ya sh.100,000 Chrispin Kilima ( 25 ) mwenyeji wa mkoa wa Arusha (katika picha) kwa kujifanya mwandishi wa habari wa Voice of America na kutumia jina la Igunza Emmanul na kutapeli Laptop na begi la mwandishi wa habari Patrick Mabula wa gazeti la Majira anayefanya shughuli zake mjini Kahama.

Kijana huyo alihukumiwa kwenda jela miezi minne au kulipa faini ya sh.100,000 lakini alishindwa kutoa faini hiyo na kwenda jela.


Akitoa hukumu hiyo jana hakimu mfawidhi wa mahakama hiyo Edina Sospeter alisema ushahidi uliotolewa na upande wa mashtaka ni kwamba pasipo shaka Kilima alijifanya mwandishi wa habari wa VoA na kutapeli laptop na begi pamoja na flash disck aliyokuwanayo mtoto wa Patrick , Emmanuel Patrick.

Hakimu Sospeter alisema ushahidi uliotolewa na mtoto Emmanuel kuwa mnamo Agosti 21,mwaka huu majira ya saa moja na nusu usiku mtuhumiwa akiwa anajitambulisha kwa kutumia jina lisilokuwa la kwake la Igunza Emmanuel alitapeli laptop ya Patrick katika ofisi yake baada ya kumrubuni mtoto wake Emmanuel kisha kutoweka nayo na kuiuza katika wilaya ya Segerema mkoani Mwanza.


Mbele ya mahakama hiyo hakimu Sospeter kwa kuzingatia ushahidi uliotolewa na shahidi wa pili wa upande wa mlalamikaji Paul Kayanda ambaye ni mwandishi wa habari wa gazeti la Uhuru ni kuwa Kilima alijifanya mwandishi wa habari wa Voice of America na kupeli laptop hiyo kwa Emmanuel.

Hakimu Sospeter alisema Kilima baada ya kutapeli laptop hiyo alikwenda kuiuza wilayani Segerema mkoa wa Mwanza kwa kiasi cha Sh.350,000/= na kisha kukimbilia wilayani Chato alikokamatwa na polisi na kuletwa wilayani Kahama kujibu kesi hiyo.

Alisema utetezi uliotolewa na mshtakiwa mbele ya mahakama hiyo ulikuwa ni wa kuidanganya kwa hiyo ameamua kumpatia adhabu hiyo ili liwe fundisho kwa watu wengine wenye tabia hiyo ya kufanya makosa ya jinai .

Akitoa hukumu hiyo hakimu Sospeter alisema mahakama imeridhika pasipo kuacha shaka na ushahidi uliotolewa na upande wa mashtaka na mashahidi Kayanda na Joseph Patrick kuwa mshtakiwa Kilima aliiba laptop hiyo na kumhukumu kwenda jela miezi minne au kulipa faini ya sh.100,000 lakini alishindwa kutoa faini hiyo na kwenda jela.

Wakiongea kwa nyakati mbalimbali baada ya hukumu hiyo wandishi wa habari wilayani Kahama walisema Kilima amekuwa akijifanya mwandishi wa habari wa vyombo mbali mbali vya nje ya nchi na ndani ya nchi na kutumia majina yao kisha kufanya utapeli wa vifaa vyao kama kamera, laptop , fedha na mabegi.

Mwenyekiti wa klabu ya waandishi wa habari wa mkoa wa Shinyanga (SPC )Kadama Malunde aliwapongeza waandishi wa habari mkoani humo kwa ushirikiano waliouonesha katika kukomesha vitendo vya watu wanaochafua tasnia ya habari kwa kujifanya waandishi wa habari.


Akiongea kwa njia ya simu ya kiganjani mwenyekiti wa klabu ya waandishi wa habari wa mkoa wa Katavi Walter Mguluchuma alisema Kilima alishafanya utapeli kama huo vifaa mbalimbali mkoani humo kwa kujifanya mwandishi wa habari na mtoto wa Seleman Kova na walishafungua jalada lenye namba MPD/RB/840/2017 na alikuwa anatafutwa na jeshi la polisi kwa tuhuma ya wizi.


Taarifa kutoka mikoa mbalimbali nchini Tanzania zinasema kuwa kijana huyo amekuwa akijitambulisha kuwa ni mwandishi wa habari wa vyombo mbalimbali vya habari vya kimataifa ikiwemo BBC,DW,VOA na kisha hujifanya kuazima vifaa vya waandishi wa habari kama vile kamera,laptop,flash disk,mabegi na kisha hutokomea kusikojulikana.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527