GODBLESS LEMA : TUNDU LISSU BADO YUPO ICU

Mbunge wa Arusha mjini Godbless Lema ambaye sasa yupo Kenya amefunguka na kueleza kuwa hali ya Mbunge wa Singida Mashariki Tundu Lissu sasa ina afadhali ukilinganisha na hali aliyokuwa nayo siku mbili zilizopita ila amedai mpaka sasa bado yupo ICU.


Lema amesema hayo alipokuwa akifanyiwa mahojiano na BBC Swahili na kudai kuwa hali ya kiongozi huyo inazidi kuimarika ukilinganisha na siku za awali ambazo alikuwa amefanyiwa shambulio hilo.


"Mgonjwa anapokuwa yupo hospitali tena kwenye chumba cha wagonjwa mahututi huwezi kusema hali ya mgonjwa ni nzuri lakini kwa kadri ambavyo tumekuwa hapa Nairobi kwa siku zote mimi na wenzangu akiwepo Mchungaji Msigwa, mke wa Lissu na Mwenyekiti wetu Freeman Mbowe tunaweza kusema kuna mabadiliko lakini bado Tundu Lissu yupo ICU na ni wito wetu kwamba Watanzania wote wenye mapenzi mema waendelee kumuombea Tundu Lissu " alisema Godbless Lema


Aidha Lema anasema kuwa jaribio la kutaka kumuuwa Lissu ni mpango na watu waliofanya hivyo siyo majambazi bali walifanya hivyo kwa lengo la kutaka kutuma ujumbe kuwa wanaweza kufanya lolote na wasifanywe jambo lolote.


Mbunge Tundu Lissu alishambuliwa kwa risasi na watu wasiojulikana Septemba 7, 2017 akiwa mjini Dodoma na baadaye kupelekwa nchini Kenya kupatiwa matibabu.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527