BARAZA LA BIASHARA SHINYANGA LABARIKI JUKWAA LA UWEKEZAJI


BARAZA la Biashara Mkoa wa Shinyanga limeazimia kufanya Jukwaa la Uwekezaji wa Biashara mwishoni mwa mwezi huu kwa lengo la kutangaza fursa za kibiashara na uwekezaji uliopo ndani ya mkoa kwa kushirikiana na Kampuni ya Magazeti ya Serikali (TSN).

Makubaliano hayo yalifanyika mwishoni mwa wiki iliyopita katika kikao cha baraza hilo kilichowakutanisha wajumbe 40 kutoka sekta za umma na binafsi, ambacho mgeni rasmi alikuwa Mkuu wa mkoa, Zainab Telack aliyewataka wajumbe wajitokeze ili kutangaza fursa zilizopo ndani ya mkoa kwa shughuli wanazozifanya.

Ofisa Mipango wa Mkoa, George Andrew aliwasilisha kwa wajumbe wa baraza hilo taarifa ya lengo la Kampuni ya TSN kuwa wako tayari kusimamia shughuli hizo za kutangaza fursa za mkoa, kinachotakiwa ni halmashauri na wadau mbalimbali kutumia jukwaa hilo kuutangaza mkoa ili jamii na wawekezaji waelewe fursa zilizopo.

“Baadhi ya halmashauri zimekwisha wasilisha taarifa zao kuhusu fursa walizonazo na kamati tendaji ya baraza la mkoa tayari tumekwisha kutembelea maeneo ya uwekezaji hayo na mrejesho tumekiwsha peleka kwenye Kampuni ya TSN kilichobaki ni sisi wenyewe kujipanga ili kuweza kufanikisha zoezi zima la jukwaa hilo,” alieleza Andrew.

Mkuu wa Mkoa, Telack alisema jukwaa hilo kuletwa mkoani Shinyanga ni fursa itakayoweza kuutangaza mkoa mambo yake yenye mafanikio ambayo baadhi ya watu hawayafahamu, lakini yapo hivyo wajumbe wa baraza walioshiriki wahakikishe wanahamasisha watu kwenye shughuli za kuona fursa na msimu wa kilimo.

“Tunafahamu azma ya serikali yetu ya awamu ya tano inayoongozwa na Rais John Magufuli kuwa tujenge uchumi wa kati na viwanda kwani mafanikio ya kuwa na uchumi wa viwanda utawezeshwa na wananchi wenye kipato cha kati ambao wataondokana na matatizo ya ujinga, umaskini na maradhi,” alieleza Telack.

Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyabiashara, Wenye Viwanda na Kilimo (TCCIA) Mkoa wa Shinyanga, Meshack Kulwa alisema jukwaa hilo litakuwa ni fursa mojawapo ya kukutana pamoja baina ya serikali, wawekezaji na wakulima, kueleza changamoto zilizopo ili kuzitatua kwa nia ya kuleta maendeleo hivyo jitihada zifanyike kufanikiwa.

Wajumbe wa kikao; Dk Ellyson Maeja na Katibu wa Chama cha Wachimbaji Wadogo Mkoa wa Shinyanga, Gregory Kibusi, walieleza kuwa jukwaa hilo chini ya uratibu wa TSN kwa kushirikiana na Mkoa na TCCIA, wamelipokea na watahakikisha fursa za mkoa kwa wafanyabiashara.

IMEANDIKWA NA KARENY MASASY, SHINYANGA

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527