TIGO YATOA MSAADA KOMPYUTA 47 CHUO KIKUU CHA DODOMA


Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Dodoma, Prof. Idris Kikula akipokea moja kati ya komputa 47 za thamani ya shilingi milioni 71/- toka kwa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tigo, Simon Karikari.Wengine kutoka kushoto Makamu Msaidizi Mkuu wa Chuo, Utawala, Mipango na Fedha, Prof. Ahmed Amme, Makamu Mkuu Msaidizi Chuo Kikuu Udom, Prof. Peter Msofe, Meneja huduma kwa jamii Tigo, Halima Okash(mwenye kilemba) na Meneja mawasiliano Tigo, Woinde Shisael. Hafla iliyofanyika jana chuoni hapo.
Meneja Mawasiliano Tigo, Woinde Shisael akizungumza na waandishi wa habari kwenye hafla ya kukabidhi komputa.
Baadhi ya wafanyakazi wa chuo kikuu Dodoma (UDOM)wakifutilia makabidhiano

****
Dodoma, Agosti 1, 2017- Kampuni inayoongoza kwa mtindo wa maisha ya kidijitali, Tigo Tanzania leo imetoa msaada wa kompyuta 47 za thamani ya shilingi milioni 71 kwa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) ili kuimarisha juhudi za taasisi hiyo za kutoa elimu ya juu nchini.


Wakati akikabidhi kompyuta hizo kwa chuo hicho Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Tigo, Simon Karikari alisema kuwa kupitia sera ya kampuni ya uwajibikaji kampuni hiyo imejikita katika kuwawezesha vijana na jamii kwa ujumla kufikia taarifa za kimataifa na uelewa, ambapo watajifunza, kupanua ubunifu wao na kushirikiana na wenzao duniani kote.


Alifafanua zaidi kuwa kupitia mchango huo, Tigo imeunga mkono Serikali ya Tanzania katika mtazamo wake wa kubadilisha nchi kuwa na uchumi unaoegemea katika uelewa ifikapo mwaka 2025 na kuthibitisha kujitoa kwa kampuni hiyo katika kuunga mkono jitihada za wizara husika ya kubadilisha elimu nchini kwa kupitia kujumuishwa kwake katika uwanja wa kidijitali.

"Kupitia uwekezaji wetu wa kijamii, Tigo imekuwa mstari wa mbele katika kukuza sekta ya elimu nchini. Hatufanyi kazi tu na taasisi za elimu ya juu, bali pia tumeshatoa kompyuta na kuunganisha zaidi ya shule 60 za sekondari kwa mtandao wa intaneti wenye kasi kupitia Mradi wetu wa Shule-elektroniki. Hali kadhalika, Tigo imetoa msaada wa madawati zaidi ya 7,100 ambayo yamewanufaisha wanafunzi wa shule za msingi zaidi ya 21,000 kote nchini ", alisema Karikari.

Mgeni rasmi katika hafla hiyo, Makamu Mkuu wa Chuo cha UDOM, Prof. Idriss Kikula alishukuru Tigo kwa mchango huo akisema; "Ni kupitia ushirikiano huu kwamba tutaweza kutoa stadi za kisasa za Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (Tehama) pamoja na maarifa kwa kizazi cha wataalamu, ili nchi iweze kukidhi mahitaji ya taarifa zinazovbadilika na mtiririko wa kidijitali katika jamii na uchumi wa dunia."

"Ninashukuru Tigo kwa utayari wake katika kushirikiana na chuo chetu ili kuongeza kiwango cha ueledi katika elimu ya kidijitali. Nakaribisha ushiriki wa wadau wengine katika utengemano wa teknolojia katika kujifunza, " alisema Kikula.

Msaada huo unafuatia mkataba wa makubaliano uliosainiwa kati ya Tigo na Chuo Kikuu cha Dodoma mwanzoni mwa mwaka huu, ambapo kampuni hiyo pia imejitolea kutoa kompyuta kwa taasisi hiyo ili iweze kutoa urahisi wa kufikiwa kwa bidhaa za mtindo wa maisha ya kidijitali za kampuni hiyo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post