NAIBU WAZIRI ATOA MAAGIZO MAZITO KWA POLISI KITENGO CHA MADAWA YA KULEVYA


Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi Mh Hamad Masauni amewaagiza askari wa Kitengo cha kudhibiti dawa za Kulevya kote nchini kuwasilisha ripoti ya ukamataji wa dawa za kulevya katika maeneo yao baada ya kubaini kuwepo kwa utendaji kazi usioridhisha.

Akizungumza mara baada ya kutembelea kitengo cha Polisi cha Kudhibiti Dawa za Kulevya kilichopo Kilwa Road Jijini Dar es Salaam, Mh. Masauni amesema kuwa, taarifa iliyopo ya ukamataji na udhibiti wa dawa hizo hauridhishi, na kutaka ripoti za maeneo mbalimbali nchini ziwasilishwe ili kupima utendaji kazi wa kitengo hicho katika kudhibiti dawa hizo zilizopigwa marufuku hapa nchini.

Mh. Masauni, amesema kuwa hawawezi kufumbia macho suala hilo kwani kuna baadhi ya maeneo yanasifika kwa kuwepo kwa dawa hizo akitolea mfano Mkoa wa Mjini Magharibi Zanzibar wenye matumizi makubwa ya dawa za kulevya lakini takwimu za udhibiti zipo chini.

Mh. Masauni amesema kuwa, Serikali inafanya jitihada za kila siku kudhibiti suala la uingizwaji, usambazaji na matumizi ya dawa za kulevya hususani maeneo ya mipakani na bandari zote kwani wanalenga kudhibiti kwa kiwango cha juu upatikanaji wa dawa hizo hapa nchini.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post