LHRC WAUNGANA NA CHAMA CHA WANASHERIA KUPINGA OFISI ZA MAWAKILI KUPIGWA BOMU DAR

Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika ‘TLS’, ambaye pia ni Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu ameendelea kulaani tukio la kuvamiwa ofisi za Wanasheria IMMMA Advocates na kusema ni muhimu jambo hilo likapigiwa kelele kwa kuwa siyo la kisiasa.

Lisu amesema hayo baada ya kualikwa katika mkutano wa kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC)na kusema kuna mashirika mengi yasiyokuwa ya kiserikali ndani ya Tanzania ambayo yanafanya kazi za kutetea haki za binadamu lakini wengi wao katika tukio hili wamekuwa wapo kimya.

"Ni muhimu sana hili jambo likapigiwa kelele maana siyo la kisiasa kama ambavyo wanayozungumza. Usalama wa Mawakili na utawala wa sheria na ulinzi wa haki za binadamu ndicho ambacho tunakisema hapa", alisema Lissu.

Pamoja na hayo, Lissu alikipongeza kituo cha LHRC kwa ujasiri waliyoweza kuonyesha kwa kujitokeza mbele hadharani na kupaza sauti yao juu ya manyanyaso wanayoyapata mawakili huku akiwashangaa baadhi ya taasisi nyingine zinazoshughulikia kutetea haki za binadamu kuogopa kuongelea hilo. 

"Wengi katika tukio hili wamenyamaza na kuogopa, kituo cha Sheria na Haki za Binadamu wamesimama hadharani na kupaza sauti zao kwa hichi kilichotokea cha kuvamiwa Mawakili. Sasa naomba nitoe pongezi za dhati kabisa kwa kituo cha haki na binadamu kwa kuwa mtetezi wa kweli kwa Mawakili wanaoshambuliwa pamoja na kuwaunga mkono Mawakili wetu katika kipindi hiki kigumu. Maana mtetezi wa kweli utamjua wakati umeshambuliwa", alisisiza Lissu.

Kwa upande mwingine, Lissu amesema mwaka huu 2017 wametunga sheria inayosema kila mtu mwenye kesi Mahakamani anastahili kupata msaada wa kisheria wa Mawakili ila anashangaa wanapowashambulia Mawakili hao.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527