MFANYABIASHARA AKIFIKISHWA MAHAKAMANI KWA KUKUTWA NA SURUALI 5,000 ZA JWTZ


Mfanyabiashara wa Kariakoo, Casto Ngogo (35) amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na mashitaka ya kukutwa na vifaa vya serikali ambavyo ni suruali 5,000 sare za Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).


Ngogo ambaye ni mkazi wa Tabata Segerea alifikishwa mahakamani hapo jana mbele ya Hakimu Mkazi, Victoria Nongwa na kusomewa mashitaka yake na Wakili wa Serikali, Hamisi Saidi.


Akisoma mashitaka, Wakili Saidi alidai Juni 15, mwaka huu maeneo ya bandari kavu ya Galco iliyopo Chang’ombe wilaya ya Temeke, Dar es Salaam, Ngogo alikutwa na suruali 5,000 za JWTZ kwenye kontena namba PCIU 82851 (5) za thamani ya Sh milioni 59 mali ya serikali bila kuwa na kibali.


Mshitakiwa alikana mashitaka hayo upande wa mashitaka ulidai kuwa upelelezi wa shauri hilo haujakamilika na kwamba hawana pingamizi ya dhamana. 


Hakimu Nongwa alitaja masharti ya dhamana kwa mshitakiwa kuwa na fedha taslimu Sh milioni 30 au hati ya mali isiyohamishika ya thamani hiyo pamoja na wadhamini wawili watakaosaini bondi ya Sh milioni 10 kila mmoja. 


Ngogo alitimiza masharti hayo na kuachiwa huru ambapo kesi hiyo imeahirishwa hadi Julai 17 mwaka huu kwa ajili ya kutajwa.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post