JELA MIAKA 20 KWA KUKAMATWA NA MENO YA TEMBO KATAVI


Mahakama ya Wilaya ya Mpanda imemuhukumu Robati Nakie 44 Mkazi wa Kijiji cha Kanoge Makazi ya Wakimbizi ya Katumba Wilayani Mpanda Mkoa wa Katavi kifungo cha miaka 20 jela baada ya kupatikana na hatia ya kukamatwa na meno ya Tembo yenye thamani ya Tshs 120,000,000 akiwa ameyapakia kwenye pikipiki .

Hukumu hiyo ilitolewa jana na Hakimu mkazi mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Mpanda Chiganga Ntengwa baada ya Mahakama kuridhika na ushahidi uliotolewa mahakamani na upande wa mashita uliokuwa na mashahidi saba .

Awali katika kesi hiyo Mwendesha mashtaka wa serikali wa mkoa wa Katavi Jamira Mziray aliiambia Mahakama kuwa mshitakiwa alitenda kosa hilo hapo oktoba 21 mwaka 2016 huko katika Jijiji cha Kanoge Makazi ya Wakimbizi ya Katumba .

Mziray alidai kuwa siku hiyo ya tukio mashitakiwa alikamatwa na Askari wa Hifadhi ya Katavi akiwa na meno ya Tembo vipande 11 vyenye thamani ya shilingi milioni 120 ambayo alikuwa ameyapakia kwenye pikipiki kwa lengo la kwenda kuyauza .

Aliiambia Mahakama kuwa kabla ya mshitakiwa kukamatwa Askari wa Hifadhi ya Taifa ya Katavi walipata taarifa za kuwa mshitakiwa Robati Nakie anamiliki kinyume cha sheria nyara za Serikali meno ya Tembo na ndipo walipoandaa mtego na kufanikiwa kumkamata mshikiwa akiwa na meno hayo ya Tembo .

Hakimu Mkazi mfawidhi Chiganga Ntengwa kabla ya kusoma hukumu aliiambia Mahakama kuwa kutokana na ushahidi uliotolewa mahakamani hapo na upande wa mashitaka ulikuwa na mashahidi watano na upande wa utetezi ambao haukuwa na shahidi hata mmoja mahakama pasipo shaka yoyote imemtia hatiani mshitakiwa Robati Nakie .

Hivyo Mahakama imemtia mshitakiwa hatiani kwa kosa la kifungu cha sheria No235 cha kanuni ya adhabu na sheria ya wanyama pori ya mwaka 2009.

Hakimu Chiganga alitowa nafasi kwa mshitakiwa kama anayosababu yoyote ya msingi ya kuishawishi Mahakama iweze kumpunguzia adhabu ambapo katika utetezi wake mshitakiwa aliiomba Mahakama impunguzie adhabu kwa kuwa anafamilia ambayo inamtegemea madai ambayo yalipingwa vikari na mwendesha mashitaka wa Serikali Jamira Mziray ambae aliiomba Mahakama itowe adhabu kali ili iwe funzo kwa wengine.

Baada ya kuzisikiliza pande hizo mbili Hakimu Chiganga alisoma hukumu hiyo na kuiambia Mahakama Mahakama imemuhukumu mshitakiwa kifungo cha miaka 20 jela kuanzia jana.
Na Walter Mguluchuma-Malunde1 blog Katavi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post