WABUNGE WAISHAMBULIA SERIKALI BUNGENI

Mbunge wa Songwe (CCM), Philipo Mulugo amesema kitendo cha Wizara ya Elimu, Teknolojia na Ufundi kuchapisha vitabu vyenye makosa kinaitia doa Serikali na kutaka watalaamu waliopo katika Taasisi ya Elimu (TIE) waangaliwe.

Akichangia bajeti ya wizara hiyo, alisema uchunguzi wake umebaini madudu mengi.

“Suala la vitabu unaweza ukalia, nimefanya uchunguzi wa vitabu ni hatari na aibu ya dunia,” alisema naibu waziri huyo wa elimu wa zamani na kuongeza:

“Kuna mambo mengine lazima tuseme Serikali ni ya kwangu, nchi ya kwangu, hatuwezi kufumbia macho.”

Naye Mbunge wa Vunjo (NCCR-Mageuzi), James Mbatia alisema Serikali ni lazima ichukue hatua dhidi ya watu ambao wanataka kuangusha elimu nchini, kwani bila vitabu bora ni vigumu kufikia malengo ya kuondoa ujinga nchini.

“Tatizo kubwa la elimu nchi hii linaanzia bungeni, tusitumie wingi wa itikadi zetu kuliua Taifa hili. Inatia uchungu kila Waziri anayeingia kwenye Wizara hiyo yeye ndio sera, mitaala na kila kitu,”alisema.

Aliongeza kuwa kama Bunge haliwezi kuisimamia Serikali ipasavyo, taifa haliwezi kufanya vizuri kielimu.

“Mwaka jana tulizungumza kuhusu vitabu, udhibiti wa vitabu ukapelekwa Taasisi ya Elimu, leo hii Serikali ya Awamu ya Tano inaandika kitabu cha Kiingereza darasa la tatu hapa juu penyewe tu pameandikwa ‘I learn English Language’ ndiyo kodi tunazopitisha zinaandika vitabu hivi?”alihoji.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post