RITA KUSAJILI WATOTO 740,000 MIKOA YA SHINYANGA NA GEITA

AWAMU ya nne ya usajili wa watoto chini ya miaka mitano katika mikoa ya Geita na Shinyanga itaanza keshokutwa katika vituo zaidi ya 650 vyenye wasajili wasaidizi wapatao 1,250.

Usajili huo unadhaminiwa na kampuni ya simu za mkononi ya Tigo kwa kushirikiana na Wakala wa Usajili, Udhamini na Ufilisi (RITA) na Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshugulikia Watoto (UNICEF).

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na RITA, Mpango huo wa usajili na kutoa vyeti vya kuzaliwa kwa watoto chini ya miaka mitano unatarajiwa kutekelezwa katika wilaya tatu mkoani Shinyanga na halmashauri zake sita; wilaya tano na halmashauri sita mkoani Geita.

Katika taarifa hiyo, Ofisa Mtendaji Mkuu wa RITA, Emmy Hudson alisema, takwimu za Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2012 zinasema asilimia 9.4 ya watoto mkoani Shinyanga na asilimia 8.6 katika Mkoa wa Geita wamesajiliwa na kupatiwa vyeti vya kuzaliwa.

Alisema, lengo la RITA chini ya mpango huo ni kusajili watoto wote 740,912 ambao hawajasajiliwa na hawana vyeti vya kuzaliwa katika mikoa yote miwili kwa kipindi cha miezi sita.

Alisema, wasajili watakuwa katika ofisi za Ofisa Mtendaji wa Mtaa na katika maeneo ambayo kinamama huenda kupata huduma za kiafya za watoto.

Meneja wa Huduma za Jamii wa Kampuni ya Tigo, Halima Okash alisema kampuni ya Tigo imekuwa mshirika mkuu wa mkakati wa usajili wa watoto wa chini ya miaka mitano.
Chanzo-Habarileo

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post