MTOTO ATAKA AKIFA AHIFADHIWE ,AFUFULIWE DAWA YA UGONJWA WAKE IKIPATIKANA

MAHAKAMA ya mjini London imetoa ruhusa kwa mwili wa binti wa miaka 14 aliyefariki kwa ugonjwa wa saratani kuhifadhiwa katika vimiminika maalumu kama alivyotaka ili kuja kuamshwa baadaye dawa za saratani anayougua itakapopatikana.

Binti huyo ambaye jina lake limehifadhiwa aliomba mahakama kumpa haki ya kuhifadhiwa kwa kuwa hataki kufa akiwa mtoto ingawa anajua ugonjwa anaougua utamuua.

Ruhusa hiyo ya kutekelezwa kwa matakwa yake imetolewa huku baba yake mzazi akiwa anapinga mtoto wake kuhifadhiwa kwa kauli kwamba hata kama ataamshwa miaka 100 ijayo au 200 atakuwa hana mtu anayemtambua ambaye ni ndugu yake.

Binti huyo ambaye aliomba nafasi ya kuhifadhiwa katika mfumo huo maalumu akisubiri kuamshwa baada ya dawa kupatikana, ombi lake lilikuwa linaungwa mkono na mama yake mzazi.

Jaji wa mahakama kuu alisema kwamba ombi la binti huyo ni vyema kusikilizwa na kwamba mama mzazi aruhusiwe kuona namna bora ya kumhifadhi binti yake. Binti huyo ambaye alikufa Oktoba mwaka huu, mwili wake tayari umeshapelekwa Marekani kwa kuhifadhiwa.

Taarifa ya shauri hilo la aina yake, ndio kwanza imetolewa na mahakama. Binti huyo ambaye hakutajwa jina lake na ambaye alikuwa anaishi mjini London, Uingereza katika siku za mwisho za uhai alikuwa anajifunza kwa bidii masuala yanayohusu hifadhi kusubiri kuamshwa baada ya dawa za ugonjwa kupatikana.

Mfumo huo ambao kiingereza unajulikana kama Cryonics (neno lililotolewa kutoka lugha ya Kigiriki) huwezesha kuhifadhiwa kwa mwili wa marehemu katika kiwango cha chini cha joto na mara nyingi ni chini ya hasi 130 sentigredi, kusubiri maendeleo ya sayansi katika ugunduzi wa dawa kwamba mwili huo utatibiwa na kuamshwa kuendelea na maisha.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post