MBUNGE GODBLESS LEMA KATIKA JARIBIO LINGINE LA DHAMANA LEO

Jaribio jingine la maombi ya dhamana ya Mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), Godbless Lema linafanyika leo baada ya kusota mahabusu tangu akamatwe mkoani Dodoma Novemba 3.


Lema anayekabiliwa na tuhuma ya kutoa lugha ya uchochezi dhidi ya Rais John Magufuli, ombi hilo la dhamana linakuwa la tatu baada ya kukwama mara mbili tangu alipoingizwa mahabusu.


Lema ambaye anatetewa na mawakili sita; Peter Kibatala, John Mallya, Charles Adiel, Adam Jabir, Faraja Mangula na Sheck Mfinanga, dhamana yake licha ya kutolewa na Hakimu Mkazi, Desdery Kamugisha ilipingwa kutokana na notisi ya rufani iliyowasilishwa na mawakili wa Serikali.


Baada ya notisi hiyo, Lema aliandika barua Mahakama Kuu kuomba mapitio ya kesi hiyo kwa maelezo kuwa taratibu za kisheria zilikiukwa kutokana na hakimu kutoa dhamana lakini akashindwa kukamilisha masharti ya dhamana na kupokea hoja za Jamhuri.


Hata hivyo, wakili mwandamizi wa Serikali, Paul Kadushi aliwasilisha pingamizi jingine kupinga Mahakama Kuu kufanya marejeo ya kesi hiyo.


Kadushi aliwasilisha hoja mbili za kisheria juu ya kuweka pingamizi la ombi la mbunge huyo kuwa muombaji hakukidhi vigezo vya kuiomba mahakama irejee maamuzi ya mahakama kwa kuwa badala ya kuiandikia mahakama barua ya kuomba ifanye mapitio ya maamuzi hayo, angetakiwa akate rufaa juu ya maamuzi ya mahakama.


Pia, alisema maombi hayo yamekinzana na Sheria ya Mahakama za Hakimu kifungu (43) (2) kutokana na mahakama hiyo kutokuwa na uwezo wa kupokea ombi ama kukata rufaa kwa maamuzi hayo, kwa kuwa ni madogo.


Hata hivyo, mawakili wa Lema walipinga hoja hizo na kueleza sheria zinaruhusu mlalamikaji kuandika barua kuomba mapitio, na tayari suala hilo limewahi kufanyika hata kwa ofisi na mwanasheria mkuu kuomba mapitio.


Wakili Kibatala alisema Mahakama Kuu ina mamlaka ya kisheria yenyewe kufanya mapitio ya kesi hata kama hakuna aliyelalamika na tayari imewahi kufanya mapitio kwa kesi kadhaa.


Baada ya hoja za pande zote kutolewa Jaji Sekela Moshi aliomba kupewa muda, kupitia hoja zote zilizoletwa na pande zote ili kuzifanyia maamuzi leo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post