WAZIRI WA HABARI AWASILISHA MUSWADA WA SHERIA YA HUDUMA ZA HABARI MBELE YA KAMATI YA BUNGE

WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye amewasilisha Muswada wa Sheria ya Huduma za Habari mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Maendeleo ya Jamii na kueleza kuwa, unalenga kuihamisha sekta ya habari kuwa taaluma kamili na kuweka masharti ya kukuza na kuimarisha taaluma na weledi katika tasnia ya habari nchini.

Aidha, amesema pia itawezesha kuundwa kwa bodi ya ithibati ya wanahabari, Baraza huru la habari pamoja na kuweka mfumo wa usimamizi wa huduma za habari, jambo litakalochangia heshima kwa tasnia hiyo na kuchangia zaidi katika maendeleo ya taifa.

Alisema muswada huo umeandaliwa kukabiliana na changamoto mbalimbali zilizopo katika tasnia ya habari nchini ambazo ni pamoja na upungufu wa sheria zinazosimamia tasnia hiyo na mabadiliko ya teknolojia ya habari.

Pia alisema changamoto ya kutokuwepo kwa udhibiti wa mzuri na usimamizi madhubuti ya viwango kwenye taaluma ya habari na utangazaji kumechangia madhila kwa jamii ikiwemo kuandikwa habari za upotoshaji, zinazokiuka maadili na zinazoweza kusababisha chuki, machafuko na uvunjifu wa amani.

‘’Hivyo kuifanya serikali na wadau wengine kuona umuhimu wa kuwa na sheria kama hii itakayoainisha bayana sifa na viwango vya kitaaluma katika tasnia ya habari. Kukamilika kwa sheria hii kutapanua wigo kwa wananchi kupata haki yao ya kikatiba ya kupata habari,’’ alisema Nape.

Alisema kutokana na mwingiliano wa teknolojia, mwaka 2003 serikali iliona umuhimu wa kuunganisha vyombo viwili; Tume ya Mawasiliano na Tume ya Utangazaji ili kuleta ufanisi wa usimamizi wa sekta na utoaji wa huduma bora kwa walaji.

“Kwa ujumla sekta hii changamoto kubwa ni taaluma ya habari kutotambulika kama taaluma kamili inayopaswa kuheshimiwa, kukosekana vyombo madhubuti na huru vya usimamizi na badala yake mambo mengi kuwa chini ya serikali moja kwa moja,” alisema na kuongeza kuwa, changamoto nyingine ni wadau wa habari kutoshirikishwa kikamilifu katika utungwaji wa sheria zilizopo, hivyo kutokidhi matakwa ya wadau katika sekta ya habari.

“Sheria hii inaleta mageuzi makubwa katika usimamizi wa sekta ya habari hapa nchini ni sheria ambayo inakwenda kwa mara ya kwanza katika historia ya nchi yetu, kuifanya rasmi sekta ya habari kuwa sekta rasmi,” alisema.

Aidha, alisema wengi wamekuwa waathirika wa uandishi usiozingatia maadili na weledi wa taaluma ya habari na utangazaji kwa kukashifiwa au kuzushiwa taarifa zisizokuwa na ukweli wowote.

Alisema mapendekezo yaliyomo katika sheria ya habari kwa kiasi kikubwa yamelenga kutatua changamoto ya kuwa na wanahabari waliosomea kazi yao na ambao wamewekeana maadili ya kufuata.

“Ni sheria itakayoleta mifumo ya kisasa ya usimamizi na ni mifumo ambayo inaweza kugusa au kubadili namna tutakavyotenda na tunavyofikiria sasa, niwaombe wanatasnia wenzangu tuwe tayari kwa mabadiliko ili taaluma yetu iheshimiwe na sisi wenyewe tuheshimike zaidi,” alisema.
 

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post