MCHUJO MPYA BODI YA MIKOPO WANAFUNZI ELIMU YA JUU BALAA



Waziri wa Elimu, Prof. Joyce ndalichako


SAKATA la wanafunzi wa elimu ya juu nchini kuendelea kusotea mikopo bado linatikisa, baada ya Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB), kusema itafanya uchunguzi kwa wanafunzi wote watakaopata mikopo kwa mwaka wa masomo 2006/17.

Taarifa iliyotolewa jana na Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Mikopo, Abdul-Razaq Badru, ilielza kuwa maombi ya mikopo 88,163 yamepokewa hadi kufikia Agosti, mwaka huu na kwamba mikopo itaanza kutolewa baada ya kazi ya uchambuzi mpya kukamilika.

Alisema katika uchambuzi huo jumla ya wanafunzi wapya 20,183 wamepangiwa kupata mikopo ambapo upangaji huo umezingatia vigezo vilivyomo katika mwongozo wa utoaji wa mikopo uliopitishwa na bodi ya wakurugezi na kuidhinishwa na Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi.

Badru alisema utaoaji huo wa mikopo unakwenda sambamba na vipaumbele vya kitaifa vinavyoendana na Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano, Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 na Mafunzo ambayo yatazalisha wataalamu wanaokidhi mahitaji ya kitaifa katika fani za kipaumbele.

Alizitaja fani hizo kuwa ni Sayansi za Tiba na Afya, Ualimu wa Sayansi na Hisabati, Uhandisi wa Viwanda, Kilimo, Mifugo, Mafuta na Gesi Asilia, Sayansi Asilia na Sayansi za Ardhi, Usanifu Majengo na Miundombinu.

“Na pia tunaangalia uhitaji wa waombaji hususani wenye mahitaji maalum kama vile ulemavu na uyatima, waombaji wanaotoka katika familia zenye hali duni ya kimaisha.

“Wadahiliwa yatima waliopata mkopo 873, wadahiliwa wenye ulemavu wa viungo 118, wenye mzazi mmoja 3,448, Wadahiliwa wahitaji waliofadhiliwa na taasisis mbali mbali 87, wadahiliwa wahitaji wanaosoma kozi za kipaumbele 6,159 pamoja na wadahiliwa wahitaji wanaosoma kozi zingine 9,867 na jumla ni wanafunzi 20,183,” ilieleza taarifa hiyo

Fedha zinazohitajika

Mkurugenzi huyo wa Bodi ya Mikopo alisema kuwa bajeti iliyoidhinishwa kwa ajili ya ukopeshaji kwa mwaka wa fedha wa 2016/17 ni Sh bilioni 483, kwa ajili ya jumla ya wanafunzi wa mwaka wa kwanza wapatao 25,717 na wanaoendelea na masomo wapatao 93, 295.

Hatua zitakazochukuliwa

Badru alisema kuwa katika taarifa yake kuwa wanufaika wote wanaopungukiwa na sifa watachunguzwa kwa ajili ya kurekebishiwa au kuondolewa katika unufaika wa mkopo.

“Waombaji waliowasilisha taarifa zenye upungufu, taarifa zao zitahakikiwa na wakibainika kuwasilisha taarifa za uongo watachukuiwa hatua stahiki ikiwa ni pamoja na kufutiwa mikopo yao.

“Wanufaika wote watatakiwa kuhuisha taarifa kwa kujaza dodoso. Taarifa za ziada za kiuchumi za wazazi au walezi wao zitatumika kutanua uhalisia. Wale watakaokutwa na hadhi zisizo stahili, watapoteza sifa za kuendelea kupata mikopo na kulazimika kurejesha kiasi watakachokuwa wamepokea tayari,” ilieleza taarifa hiyo.

Juzi Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiwa kwenye maadhimisho ya miaka 55 ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), alisema suala la mikopo kwa wanafunzi wa walimu ya juu tayari Rais Dk. John Magufuli ameshatoa ufafanuzi wa kina kwa wizara juu ya namna ya utoaji wa mikopo.

Aliwataka waombaji kushirikiana na Wizara ya Elimu, katika kutoa taarifa zao sahihi ili kurahisisha utoaji wa mikopo.

Hata hivyo, Majaliwa alisema Serikali ilikwishaongeza bajeti ya mikopo ya elimu ya juu kutoka Sh bilioni 340 mwaka 2015/2016 hadi sh. bilioni 483 kwa mwaka 2016/2017.

“Taarifa niliyoipata leo (jana) ni kwamba tayari wanafunzi wameanza kulipwa kwa uchache na kwamba kufikia kesho kutwa (kesho) asilimia 90 ya wanafunzi wanaostahili kulipwa watakuwa wamepata fedha zao,” alisema Majaliwa.

Pia aliwataka watumishi wa Bodi ya Mikopo kutekeleza majukumu yao kwa wakati na kwamba serikali haitavumilia tena ucheleweshaji wa mikopo kwa wanafunzi.

“Ni muhimu pale panapoonekana kuwapo kwa tatizo, taarifa ndani ya serikali zitolewe haraka ili kuzuia migogoro isiyo ya lazima kati ya wanafunzi na Serikali yao,” alisisitiza Majaliwa.

CHANZO-MTANZANIA

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527