KIZIMBANI KWA KUTISHIA KUUA WATOTO KWA KUWAPA SUMU



MKAZI wa Mwananyamala jijini Dar es Salaam, Mwenda Saidi (40), amepandishwa kizimbani katika mahakama ya Mwanzo Kinondoni, kwa madai ya kutishia kuua watoto wa sumu. Imedaiwa mahakamani kuwa, mshitakiwa alitishia kuua watoto wa Ismael Iddi.

Msoma mashitaka, Rukia Liganduka, amedai mbele ya Hakimu Ester Kilio, kuwa, mshitakiwa alitenda kosa hilo, Oktoba 9 saa 11 jioni, Mwanyamala wilaya ya Kinondoni.

Liganduka amedai kuwa, mshitakiwa huyo alisema kuwa, atawatilia sumu kwenye chakula watoto wa Ismail huku akijua kufanya hivyo ni kosa kisheria.

Saidi amekana mashitaka, kesi hiyo inatarajiwa kusomwa tena Novemba 1, mwaka huu.

Katika kesi nyingine, dereva pikipiki maarufu kama bodaboda, Ally Judi amepandishwa kizimbani mahakamani hapo kujibu mashitaka ya wizi baada ya kukabidhiwa pikipiki MC 348 AJG aina ya Fekon yenye thamani ya laki tisa.

Liganduka amedai mahakamani kuwa, mshitakiwa alitenda kosa hilo Septemba 25 , 2016, saa 4 asubuhi eneo la Msasani Namanga, wilaya ya Kinondoni.

Msoma mashitaka amedai kwamba mshitakiwa alikabidhiwa pikipiki hiyo na Zuhura Mwedadi kwa ajili ya kufanya kazi ya kubeba abiria, hatimaye alitoweka nayo hadi alipokamatwa 14 Oktoba , mwaka huu, akiwa hana chombo hicho cha usafiri.

Kwa mujibu wa Liganduka, alipoulizwa mshitakiwa huyo hakusema pikipiki ilipo, wakati alijua kufanya hivyo ni kinyume cha sheria.

Kesi hiyo imeahirishwa na itatajwa tena Novemba 1, mwaka huu.

Imeandikwa na Mohamed Mussa-Habarileo

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527