ACT WAZALENDO YAJIBU MASHAMBULIZI YA CCM KUHUSU ZITTO KABWE


Chama cha ACT-Wazalendo kimesema kimeshtushwa na tuhuma dhidi ya kiongozi wake wa chama, Zitto Kabwe kwamba ana miliki mali za kifisadi pamoja na kuhusishwa na ununuzi wa ardhi maeneo ya Kigamboni uliofanywa na NSSF kwa bei ya milioni 800 kwa ekari moja, wakati bei halisi ni milioni 25 na kwamba kitendo hicho kimeitia hasara serikali .

Tuhuma hizo zilitolewa jana na Msemaji wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Christopher Ole Sendeka, ambapo alivitaka vyombo vya uchunguzi kufanya uchunguzi katika shirika hilo ili kubaini waliohusika kwa ajili ya kuchukuliwa hatua za kisheria, huku akimhusisha Zitto katika uchunguzi huo.

Ole Sendeka alitaka akaunti za benki za Zitto pamoja na maisha yake binafsi kuchunguzwa kama yana uhalisia na kipato chake halali.

Tuhuma hizo zimekiibua chama cha ACT, ambapo leo Katibu wa Bunge na Serikali za Mitaa ACT, Habibu Mchange amevitaka vyombo vya uchunguzi haraka iwezekanavyo kuchunguza mali, madeni, akaunti zote za benki pamoja na mfumo wa maisha ya Zitto.

“ACT imeshtushwa na tuhuma, kashfa, porojo na matusi mbalimbali yaliyotolewa jana na Ole sendeka dhidi ya kiongozi wa chama chetu,” amesema.

Amesema kuwa, katiba ya chama hicho huwataka viongozi wote kuweka hadharani matamko ya mali zao na madeni na kwamba Zitto alitekeleza matakwa hayo ya kisheria hivyo mali na madeni yake yako hadharani na mtandaoni.

“Tunaamini kama kuna kiongozi ambaye mali, madeni, maslahi, na akaunti zake viko wazi basi ni ndugu Zitto,” amesema.

Aidha, Mchange amedai kuwa, kilichomsukuma Sendeka kutoa tuhuma hizo kwa Zitto ni harakati zake za kuupinga muswada mpya wa habari.

“Tuhuma za ole sendeka kuna kitu nyuma yake, jitihada za zito za kupambana na mswada wa habari ndizo zilizomuibua, sababu wanataka upitishwe ili kuviua vyombo vya habari,” amesema.

Amesema ACT itaendelea kuisimamia serikali katika mambo ya bungeni kama anavyofanya mbunge na kiongozi wao wa chama.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527