Picha 15!! Makaburi Yafukuliwa Shinyanga,Viungo Vya Binadamu Vyaokotwa Mtaani,Mbwa Wakutwa Juu ya Makaburi Wakila Viungo Vingine


Kumetokea tukio la aina yake leo katika manispaa ya Shinyanga ambapo viungo vya miili ya binadamu waliozikwa katika makaburi ya watu wasiokuwa na ndugu vimeokotwa mtaani majira ya saa moja asubuhi na kuwaacha midomo wazi wakazi wa eneo hilo.


Malunde1 blog,Fahari ya Shinyanga huwa haipitwi na matukio,mwandishi mkuu wa mtandao huu ,Kadama Malunde amefika katika eneo la tukio na kujionea hali halisi ilivyokuwa makaburi ya Mageuzi maarufu makaburi ya Dodoma,...Anaripoti


Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo wamesema viungo vya miili ya binadamu vimeokotwa katika mtaa wa Butengwa kata ya Ndembezi baada ya makaburi ya watu wasiokuwa na ndugu yaliyopo katika mtaa wa Mageuzi kata ya Ngokolo katika manispaa ya Shinyanga kufukuliwa na fisi.


Akielezea kuhusu tukio hilo mjumbe wa serikali ya mtaa wa Butengwa Peter Joseph ambako vipande vya miili ya binadamu imeokotwa alisema alipewa taarifa kuwa kuna miili ya binadamu katika mtaa wake uliopo jirani na makaburi hayo umbali wa mita 300.

“Nikiwa na wananchi wa mtaa tulishuhudia kipande cha mkono wa binadamu kikiwa kimeliwa vidole,ambapo mwanzo tulidhani ni mfupa wa mguu wa ng’ombe (kongolo),nikawasiliana na viongozi mtaa wenzangu na mtaa wa jirani na polisi,tukaenda kujiridhisha kwenye makaburi tukakuta mbwa sita wakiwa juu ya makaburi wakila viungo vya binadamu huku makaburi yakiwa wazi”,alieleza Joseph.

“Tulishangaa kuona mbwa wakitafuna miili ya binadamu,hatukuona utumbo kwani walikuwa wameshatafuna tlichokiona ni vipande vya miili ya binadamu zikiwemo mbavu na kipande cha mkono wa binadamu huku vipande vingine vya mwili vikiwa kaburini vikivuja damu huku vikiwa vimefunikwa na mfuko wa sandaruri”,aliongeza Joseph.

Alisema wiki iliyopita waliona magari ya serikali ya manispaa ya Shinyanga yaliyoleta miili ya marehemu ambao hawana ndugu na mara nyingi watu wasio na ndugu huwa wanazikwa na watu wanaolipwa na serikali ambao hufanya kazi haraka haraka na kondoka.

Naye mjumbe wa serikali ya mtaa wa Mageuzi kata ya Ngokolo yalipo makaburi hayo Mhoja Pius aliyemwakilisha mwenyekiti wa mtaa alisema tukio hilo linatokana na uzembe wa halmashauri ya manispaa ya Shinyanga kutosimamia vizuri mazishi ya watu wasiokuwa na ndugu.

“Haiwezekani kaburi la binadamu liwe na urefu wa futi moja halafu inavyoonekana watu zaidi ya mtu mmoja wamezikwa katika kaburi moja,wiki iliyopita tuliona gari la magereza na jingine la manispaa ya Shinyanga walikuja kuzika,pengine waliozikwa hapa ni wafungwa”,alisema Pius.

“Mara nyingi manispaa wakija kuzika huwa hawatoa taarifa kwa viongozi wa serikali ya mtaa,hili tukio la miili ya binadamu kufukuliwa ni la pili jingine lilitokea mwaka 2012 tulikuta mtu kazikwa huku mkono wake ukiwa nje ya kaburi tukashirikiana na wananchi kufunika kaburi”,aliongeza Pius.

Mjumbe mwingine wa mtaa wa Mageuzi aliyefika eneo la tukio Sada Bakari  alisema baada ya polisi kufika eneo la tukio waliwaruhusu wananchi kufukia makaburi mawili yaliyokuwa wazi huku miili ya binadamu ikionekana.

Aliongeza kuwa katika makaburi hayo yenye urefu usiozidi hata kwenye magoti ya binadamu wamezikwa watu zaidi ya mmoja na kwamba kuna taarifa kuwa waliozikwa katika makaburi hayo ni wafungwa.

Naye mmoja wa wakazi wa mtaa wa Mageuzi Jofrey Rugalema alieleza kusikitishwa na tukio hilo na kuutaka uongozi wa manispaa ya Shinyanga ithamini binadamu hata kama hawana ndugu kwani ni aibu na fedheha kubwa mizoga ya binadamu kuokotwa mtaani.

“Huu ni uzembe wa hali ya juu haiwezekani binadamu azikwe kwenye kaburi la urefu wa futi tatu,usimamizi wa mazishi ya watu wasio na ndugu ni mbovu,kinachokera zaidi pamoja na kupigiwa simu hakuna hata kiongozi mmoja wa manispaa aliyefika katika eneo la tukio,polisi ndiyo wamefika mapematu baada ya kuwapa taarifa”,alisema Rugalema.

Akizungumza na Malunde1 blog Kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga Mika Nyange alisema baada ya kupata taarifa za kuwepo kwa tukio hilo walifika na  kubaini kuwa makaburi hayo yamefukuliwa na fisi.

“Kutokana na kwamba manispaa ya Shinyanga ndiyo wanahusika na makaburi hayo kwa mujibu wa sheria na taratibu tumekubaliana washirikiane na wananchi kuzika upya miili ya marehemu ambao wamezikwa katika maburi yaliyofukuliwa na fisi”,alieleza Kamanda Nyange.


Malunde1 blog imemtafuta mkurugenzi wa manispaa ya Shinyanga Lewis Kalinjuna kuzungumzia tukio hilo lakini mpaka sasa simu yake haipatikani na juhudi za kumtafuta zinaendelea.
Kauli ya Diwani wa Kata ya Ngokolo Yalipo Makaburi>>Bofya HAPA<<
Vipande vya mwili wa binadamu vilivyookotwa katika mtaa wa Butengwa kata ya Ndembezi jirani na makaburi ya mtaa wa Mageuzi yaliyopo katikakata ya Ngokolo katika manispaa ya Shinyanga-Picha na Kadama Malunde-Malunde1 blog

Kushoto ni vipande vya nyama zinazodaiwa kuwa kuwa ni vya binadamu,kulia ni mojaya makaburi mawili yaliyofukuliwa,kinachoonekana ni vipande vya mwili wa binadamu vikiwa vimefunikwa mfuko wa sandarusi katika makaburi ya Mageuzi yaliyopo katika kata ya Ndembezi katika manispaa ya Shinyanga

Wananchi wakioneshana kaburi jingine lililofukuliwa,ambapo ndani kulikuwa na mfupa uliokauka
Viungo vya binadamu vikiwa kaburini

Wananchi wakifukia makaburi hayo

Mifupa inayodaiwa kuwa ni ya binadamu iliyookotwa kwenye makaburi hayo
Mwananchi akiwa amebeba vipande vya mifupa kwenye koleo

Wananchi wakiendelea kuokota mifupa makaburini

Mfupa ukiwa kwenye majani makaburini
Wananchi wakiondoka makaburini baada ya kuzika/kufunika miili ya binadamu kwenye makaburi yaliyokuwa wazi

Viongozi wa mtaa wa Mageuzi na Butengwa na wananchi wakitafakari jambo makaburini

Kushoto ni mjumbe wa serikali ya mtaa wa Mageuzi kata ya Ngokolo yalipo makaburi hayo Mhoja Pius akisikiliza kwa makini maelezo kutoka kwa mjumbe wa serikali ya mtaa wa Butengwa Peter Joseph ambako vipande vya miili ya binadamu imeokotwa
Mjumbe wa serikali ya mtaa wa Mageuzi kata ya Ngokolo yalipo makaburi hayo Mhoja Pius akizungumza na Malunde1 blog

Kushoto ni mjumbe wa serikali ya mtaa wa Mageuzi kata ya Ngokolo yalipo makaburi hayo Mhoja Pius akiteta jambo na mjumbe wa serikali ya mtaa wa Butengwa Peter Joseph ambako viungo vya binadamu imeokotwa

Mkazi wa eneo hilo Onesmo Omari akielezea kuhusu tukio hilo
Picha zote na Kadama Malunde-Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post